• Nairobi
  • Last Updated April 24th, 2024 5:39 PM
NGILA: Pesa zilizoibwa na kufichwa ughaibuni zirejeshwe na serikali

NGILA: Pesa zilizoibwa na kufichwa ughaibuni zirejeshwe na serikali

NA FAUSTINE NGILA

RIPOTI ya Shirika la Kitaifa kuhusu Utafiti wa Uchumi kutoka Amerika iliyotolewa juma lililopita kuwa Kenya ni ya pili duniani katika orodha ya mataifa yenye matajiri walioficha matrilioni ya pesa ughaibuni inasikitisha mno.

Licha ya serikali kuweka mikakati ya kutwaa fedha zilizopatikana kwa njia za ufisadi na ukwepaji wa ushuru, bado kuna Sh15 trilioni zilizochumwa nchini na kufichwa na mabwanyenye katika mataifa ya nje.

Changamoto ya matajiri kuficha ukwasi wao kwenye mataifa ya kigeni inakumba mataifa mengi yanayoendelea, lakini hali ya Kenya kuibuka katika mstari wa mbele kwa uovu huo ni jambo hatari kwa uchumi wetu na Afrika Mashariki kwa jumla.

Wakati Waziri wa Fedha Henry Rotich kwenye Sheria ya Fedha 2016 alitoa mwanya wa kuwaongezea muda Wakenya wenye mali ughaibuni kuirudisha nchini, alifikiri angewashawishi kutoa fedha zao kutoka mataifa ya Bermuda, Switzerland, Cayman Islands, Channel Islands na Isle of Man na kuzirudisha nchini.

Hilo halikufaulu na sasa ni wakati wa kubuni mikakati mingine itakayozaa matunda hasa ikizingatiwa kwamba fedha hizo ni mara tano ya bajeti yetu ya sasa, na zikiwekezwa vizuri hapa nchini, deni la Sh5 trilioni linalotukodolea macho litakuwa historia.

Serikali ina jukumu la dharura la kuzidisha juhudi za kurudisha matrilioni hayo ya pesa humu nchini. Hili linawezekana kwa kuunda vishawishi vya kuwachochea matajiri hawa kurudisha fedha hizo humu nchini kwa hiari yao.

Hazina kuu

Ikiwa hilo litashindikana, basi Hazina Kuu haitakuwa na budi kuwalazimisha mabwanyenye hawa kurudisha mali hiyo, kwa kuwawekea vikwazo vya kifedha.

Hatua ya pili inafaa kuhusisha ushirikiano wa serikali yetu na serikali za mataifa ambako utajiri huo umefichwa kwa kutia saini mikataba ya usaidizi kuhusu fedha hizo kama ule wa Rais Uhuru Kenyatta na mwenzake wa Switzerland Alain Berse mnamo Julai.

Kukosa kuchukua hatua za dharura kuhusu utajiri wa njia za mkato utazidisha kiburi kwa matajiri wanaotambua ufisadi kama ngao, na watazidi kujitajirisha kinyume cha sheria huku Wakenya wakiumia.

Iwapo serikali itachukua hatua mapema, basi mwendendo wa baadhi ya Wakenya kujizolea mabilioni ya pesa kutokana na ufisadi, ukwepaji kulipa ushuru na wizi wa fedha za umma utakoma.

Ni kinaya kikubwa kwa watu wachache nchini kumiliki fedha ambazo ni mara tatu ya deni tunalodaiwa na mataifa ya kigeni huku serikali ikishindwa kufadhili bajeti ya Sh3 trilioni pekee.

You can share this post!

TAHARIRI: Tulinde watoto dhidi ya maovu

ONYANGO: Raila achunge sana asiwe mwathiriwa wa referenda

adminleo