• Nairobi
  • Last Updated April 24th, 2024 1:35 PM
UNESCO kulinda muziki wa Reggae kimataifa

UNESCO kulinda muziki wa Reggae kimataifa

VALENTINE OBARA na AFP

MUZIKI wa reggae umepata ulinzi mkuu wa kitamaduni baada ya kutambuliwa na shirika la Umoja wa Mataifa linalosimamia masuala ya Elimu, Sayansi na Utamaduni (UNESCO) kama utamaduni unaopaswa kuhifadhiwa.

Kwa mujibu wa UNESCO, muziki wa Reggae, ambao mizizi yake ni Jamaica, unastahili kulindwa na kukuzwa kwa sababu ya mchango wake kwenye midahalo ya kimataifa kuhusu ukiukaji wa haki, mapinduzi, upendo na utu.

Shirika hilo lilieleza kwenye taarifa kwamba Reggae, ambayo pia ina ushabiki mkubwa Kenya, ina misingi ya kijamii, kisiasa na kiimani.

Wakati huo huo, tamaduni za jamii ya Wamaasai za Enkipaata, Eunoto na Olng’esherr sasa zitalindwa kimataifa zisiangamie baada ya kuzitambua

Tamaduni hizi za kuingiza wavulana kwa utu uzima zimetambuliwa kama zinazostahili kulindwa kwani zimo kwenye hatari ya kumalizwa na mienendo ya maisha ya kisasa.

Kutambuliwa kwa tamaduni hizi ni heshima kubwa kwa jamii ya Maasai, ambayo imefanikiwa kwa kiwango kikubwa kuliko zingine nchini kulinda tamaduni zake.

Tamaduni hizo sasa zimeingia kwenye orodha moja na densi ya Isikuti ya jamii za Isukha na Idakho kutoka Magharibi mwa Kenya, ambayo ilitambuliwa mnamo 2014, na tamaduni za Kaya katika jamii za Mijikenda zilizoidhinishwa na UNESCO mwaka wa 2009.

Uharibifu wa tamaduni au sehemu zinazolindwa na UNESCO huwa unaweza kupelekea mtu kuadhibiwa kwa msingi wa sheria za kimataifa, ikiwemo kufunguliwa mashtaka katika Mahakama ya Kimataifa ya Uhalifu (ICC).

Wakati Reggae ilipoanza kuchipuka, ilisifiwa kama muziki wa watu wanaokandamizwa kwani maneno ya nyimbo hizo yalihusu masuala ya siasa za kijamii, watu kufungwa gerezani bila hatia, na ukosefu wa usawa katika jamii.

Miongoni mwa wasanii waliopatia muziki huu umaarufu ulimwenguni ni Bob Marley, Mighty Culture, Burning Spear na Lucky Dube aliyekuwa raia wa Afrika Kusini.

UNESCO huwa inalinda sanaa na tamaduni nyingine zaidi ya 300 zikiwemo zinazohusu mapishi ya kitamaduni na hija za madhehebu ya kidini.

You can share this post!

Matatu zafungiwa nje ya katikati ya jiji, wakazi kuhangaika...

Pasta taabani kumlaghai Mjapani Sh1.2 milioni za kueneza...

adminleo