Dondoo

Buda akauka mate mdomoni baada demu kumtema ghafla

Na JANET KAVUNGA October 1st, 2024 Kusoma ni dakika: 1

SHANZU, MOMBASA

JOMBI wa hapa amebaki hoi baada ya kushindwa kulipa mkopo aliochukua kununulia demu wake gari kisha mwanadada huyo akamtema na kuhama pwani.

Biashara ya jamaa iliporomoka akawa hawezi kulipa mkopo huo huku juhudi za kumpata demu aweze kutwaa gari hilo auze aokoe jahazi zikigonga mwamba.

Kilichomramba jamaa ni kuwa, gari limesajiliwa kwa jina la kipusa huyo na hana chochote cha kuonyesha alihusika kulinunua.

Benki iliyomkopesha pesa ilimwandamana na kuuza ploti yake aliyotumia kama dhamana kwa mkopo huo. Inasemekana kuwa baada ya demu kuona biashara ya jamaa ikiporomoka, alihamia kusikojulikana.

Jamaa anajuta kuwekeza katika demu akidhani alikuwa akimpenda kwa dhati. Amekuwa akiapa kwa marafikize kwamba heri sasa asalie kapera akisema hatawahi kuamini kidosho mwingine maishani mwake.