Habari

Oburu: Huku Luo Nyanza wimbo ni tutam

Na GEORGE ODIWUOR July 13th, 2026 Kusoma ni dakika: 2

VIONGOZI wa ODM Luo Nyanza wameapa kuwa ‘watakufa’ na Rais William Ruto hadi 2027 kutokana na uimarishaji wa miundomsingi eneo hilo.

Wakiongozwa na Seneta wa Siaya, Dkt Oburu Oginga, walisema ODM haina nia ya kuwa na mgombeaji wa urais 2027 na ni Rais Ruto ndiye atapigiwa kura mwakani.

Kulingana naye, wagombeaji wengine kama Rigathi Gachagua, Martha Karua, Justin Muturi na wengine hawana nafasi ya kushinda urais.

“Wanapambana na kujipiga kifua na hata hawajaamua nani ni mgombeaji wao wa urais. Sisi tunajua nani atakuwa mgombeaji wetu na tutawashinda,” akasema.

Dkt Oginga alisema Luo Nyanza ilitengwa na tawala za nyuma kutokana na msimamo wake wa kisiasa lakini ushirikiano kati ya UDA-ODM umebadilisha eneo hilo kimaendeleo.

“Hatubaguliwi tena, tuko serikalini na tunajua mahali tunaelekea. Tuliingia kupitia dirishani lakini sasa tunajua mahali tunaenda,” akasema Dkt Oginga.

Aliwataka wakazi wa Nyanza kuwachagua viongozi wa ODM pekee ili chama hicho kiendelee kuwa na umaarufu mkubwa wa kisiasa.

“Nikiketi na Rais Ruto baada ya uchaguzi wa mwaka ujao, atauliza nina watu wangapi. Kwa hivyo, wapigie wawaniaji wa ODM viti vingine lakini urais tunampa Ruto,” akasema. Alikuwa akiongea katika ibada ya kanisa Kaunti ya Homa Bay.

Aliandamana na Katibu katika Wizara ya Usalama wa Ndani Raymond Omollo, Katibu wa Afya Ouma Oluga, Seneta wa Homa Bay Moses Kajwang na Mbunge wa Homa Bay mjini Opondo Kaluma.

Mwenyekiti wa ODM Gladys Wanga alisema eneo la Ziwa limepata maendeleo makubwa kupitia miradi ya maendeleo, akibainisha kuwa miradi ya ujenzi wa barabara inayoendelea imebadilisha kwa kiasi kikubwa sura ya eneo hilo.

“Tunaposema tunaiunga mkono serikali, si bure. Ni kwa sababu ya umoja wa Wakenya.. Hilo ndilo jambo ambalo serikali jumuishi imefanikiwa kulitekeleza,” alisema Bi Wanga.

Pia alitetea Tume Huru ya Uchaguzi na Mipaka (IEBC) dhidi ya mashambulizi ya kisiasa wakati tume hiyo ikijiandaa kuendesha uchaguzi mdogo wa Ol Kalou.

Kwa upande wake, Seneta Moses Kajwang’ alisema kuwa kwa muda mrefu wapigakura wa eneo la Ziwa waliamini kuwa maendeleo yangewezekana tu iwapo mmoja wao angekuwa kiongozi wa taifa.

Hata hivyo, alisema Kenya haihitaji kiongozi wa kieneo bali mwenye mtazamo wa kitaifa.

“Tutaendelea kuiunga mkono serikali. Ukweli kwamba tunataka kushika mamlaka haumaanishi hatutashirikiana na serikali,” akasema seneta huyo.