• Nairobi
  • Last Updated March 28th, 2024 9:35 PM
MENENGAI CRATER: Mali asili inayofumbiwa macho na serikali

MENENGAI CRATER: Mali asili inayofumbiwa macho na serikali

NA RICHARD MAOSI

KULINGANA na utafiti uliofanywa na shirika la Umoja wa Mataifa kuhusu Mazingira (UNEP), kati ya miaka ya 1990-2010 Kenya imekuwa ikipoteza asilimia 0.32 ya misitu kila mwaka, kutokana na shughuli za kibinadamu.

Hali yenyewe imeendelea kupunguza kiwango cha maliasili, hasa pale tunaposhuhudia miti iliyokomaa ikigeuzwa majivu kwa muda mfupi.

Japo serikali imejaribu kila mbinu kuweka kanuni imara za kudhibiti ukataji miti na kutoa uhamasisho kwa jamii, bado kuna mashaka makuu.

Msitu wa Menengai Crater ukiteketea na kuhatarisha maisha ya wakazi wanaozunguka msitu huo. Picha/Richard Maosi

Kubana vibali ama kuwakamata wahalifu wanaochoma makaa porini haitoshi. Huenda labda maafisa wa misitu watalazimika kubadilisha mbinu za kushika doria.

Taifa Leo Dijitali ilipozuru msitu wa Menengai Crater, ilipata maliasili inayoelekea kuangamia baada ya ushirikiano kati ya raia na maafisa wa usalama kuulinda kutozaa matunda.

Msitu wa Menengai katika Kaunti ya Nakuru unazungukwa na wakazi wanaotegemea bidhaa zinazotokana na miti kama vile mbao, makaa na asali. Ni mlima wenye kasoko (volkano) kileleni.

Daniel Ole Kuntai (kulia) mfugaji wa kuhamahama kutoka Gilgil akielezea masaibu anayopitia akitafutia lishe mifugo wake tarehe 2, Februari 2019. Picha/Richard Maosi

Unapatikana mwendo wa kilomita 10 hivi kutoka mjini Nakuru karibu na eneo la Milimani, mkabala na Olo Rongai katika upande wa Magharibi .

Vilevile, kuna baadhi ya miradi ya serikali iliyostawishwa ndani ya Menengai, mojawapo ikiwa ni mitambo ya kutuma mawimbi ya mawasiliano kwa vituo vya redio na televisheni, na pia uzalisha kawi ya mvuke (Geothermal Power).

Licha ya kutumika kama kituo cha utalii, wageni wengi humiminika hapa kutazama spishi mbalimbali za mimea , wanyama na ndege ingawa taswira ya Menengai Crater imechakaa kinyume na zamani iliposheheni uzuri wa rangi ya kijani kibichi.

Mwendeshaji bodaboda akisafirisha makaa kuelekea eneo la Subukia. Biashara hii imenoga mjini Nakuru. Picha/Richard Maosi.

Pametengwa sehemu maalum ya wageni kubarizi ili kufurahia mazingira tulivu yasiyokuwa na shughuli nyingi kila siku za wiki, lakini hata hivyo bali na uzuri wote huu visa vya moto vimekuwa ni jinamizi la kila mwaka.

Mnamo 2015, ekari 400,000 ya miti iliteketea .Waziri wa Mazingira kaunti ya Nakuru Richard Rop alisema moto huo ulisababishwa na kiangazi pamoja na upepo mkali uliosambaza moto katika sehemu kubwa.

Changamoto kubwa ikiwa ni ukosefu wa vifaa vya kisasa vya kuzima moto.

Mradi wa serikali wa kuzalisha kawi ya mvuke unaoendeshwa ndani ya msitu wa Menengai. Picha/Richard Maosi

Kulingana na wakazi wanaoishi karibu na msitu wa Menengai, serikali imekuwa ikifumbia macho jambo hili huku baadhi ya watu wakipendekeza mitaro ichimbwe ili kuzuia moto kuenea.

Upekuzi wa Taifa Leo Dijitali kwa mbali ulishuhudia moshi ukifuka angani kutoka kwenye vichaka, ila hatungeweza kufika katika sehemu yenyewe kutokana na miinuko ya ardhi.

Allan Kibor, mkazi wa Crater anasema moto umekuwa ukizuka kutokana na mambo madogo kama vile uvutaji sigara.

Ndege la Shirika la Huduma za Misitu (Kenya Forest Service) lilipotua kudhibiti hali ya moto. Picha/Richard Maosi

Baadhi ya wakazi wamekuwa wakipuuza na kutupa sigara kabla haijazima kwenye nyasi zilizokauka bila kufahamu ingeleta madhara makubwa baadaye.

Pia analaumu kampuni ya GDC inayozalisha kawi ya umeme , kwa kutumia vilipuzi akiamini huenda vimekuwa vikichochea na kuanzisha cheche zo moto .

Uchomaji msitu wa Menengai umekuwa ukifanya mifugo kukosa malisho, Wafugaji wakilazimika kutembea mwendo mrefu kutafutia ng’ombe wao nyasi na maji.

Afisa wa kulinda misitu akiwa kazini. Picha/Richard Maosi

“Endapo hali itaendelea kuwa hivi miaka nenda miaka rudi sehemu hii ambayo wakati mmoja ilisheheni miti itakuja kugeuka jangwa,”alisema.

Charles Kemita ni mmiliki wa hoteli ya kitalii ndani ya Menengai Crater kwa zaidi ya mwongo mmoja sasa.

Anasema amekuwa akishirikiana na jamii kwa mambo mengi hasa ijapo nafasi ya kutoa ajira kwa vijana wanaoishi karibu na Menengai Crater.

Wakazi wenye wasiwasi wakitazama makazi yao yaliyoteketezwa na moto katika msitu wa Menengai. Picha/Richard Maosi

Kinachomtia hofu ni kuwa biashara imeshuka maana watalii wengi hawatembelei eneo hili la kivutio kama awali .

“Mikahawa iliyokuwa ikisheheni wageni sasa imebaki kuwa mahame,”alisema.

Badala yake wageni wamenza kuzuru sehemu nyingine kama vile Nyahururu,Naivasha na Baringo kujivinjari.

Utalii ulivyokwamishwa na moto unao enea kwa haraka na kuwafanya wageni kujivinjari kwingine. Picha/Richard Maosi

“Hali ya kiangazi pamoja na familia za wafugaji wa kuhamahama ndio chanzo cha masaibu yetu, kila mwaka moto unapozuka. Japo idara husika inafahamu hili hawajachukua hatua yoyote,” alisema.

Fred Ogombe anayesimamia msitu wa Mau , alitupambanulia kwa kina hali halisi akisema kila mwaka msitu wa Menengai umekuwa ukishika moto.

“Japo ni vigumu kubaini chanzo moja kwa moja, wenyeji ndio wa kulaumu kwani wamekuwa wakiwaficha wahalifu wanaofanya biashara ya kuuza makaa,” alisema.

Sehemu ya msitu wa Menengai iliyochomeka. Picha/ Richard Maosi

Hata hivyo anasifia juhudi za serikali ya kaunti kuwasaidia wakazi kuzima moto kila mara mkasa unapotokea.

Anaamini wamekuwa nguzo muhimu sio tu kuwashauri bali pia kuchukua hatua ya haraka mkasa wa moto ukiripotiwa .

Kaunti imekuwa ikitoa magari na ndege kufikia sehemu zisizofikika ili kudhibiti makali ya moto ambao umekuwa ukiwalemea wakazi kuuzima.

Maafisa wa KFS wakitoka kutathmini kiwango cha uharibifu uliosababishwa na moto. Picha/ Richard Maosi

Jambo hili lilifanya waziri wa mazingira wa kitaifa Keriako Tobiko kufanya ziara ya ghafla kwenye msitu wa Menengai mnamo Februari 2,2019 kutathmini hali.

Akishirikiana na maafisa wa misitu(Kenya Forest Service)walitembelea msitu wa Menengai na baadaye kuzungumza na wakazi.

Ilibainika moto umekuwa ukisababishwa na wachomaji makaa ambao wamefanya misitu kuwa makao yao ya muda.

Maafisa wa KFS wasemezana baada ya kuzima moto. Picha/ Richard Maosi

Kando na kupatiwa ulinzi na maafisa wa usalama, wao huchoma makaa peupe.

Wakazi wanasema biashara ya kuuza makaa ilikuwa imenoga katika eneo la Subukia, Solai na Lanet.

Aidha wazima moto wamekuwa wakichukua muda mrefu kufika kwenye eneo la mkasa kutokana na mabonde ya kina kirefu.

Tobiko alihimiza vijana kushirikiana na viongozi wa mtaa kuanzisha mchakato wa kupanda miti tano kila mmoja ili kufikisha asilimia 10 inayohitajika.

Waziri wa Mazingira Keriako Tobiko akitathmini hali katika msitu wa Menengai ambao uliteketea siku nne mfulululizo Februari 2019. Picha/Richard Maosi

“Serikali haitalegeza vita dhidi ya ukataji miti kiholela, kwa sababu ndio chanzo cha mito na mvua”aliongeza

Misitu mingine iliyo kwenye hatari ya kuangamia ni kama vile Narasha (Baringo), Ndoinet, Olposimoru , Sabatia, Eburru (Nakuru), Londiani (Kericho) na Olrabel (Baringo).

“Baadhi ya misitu inateketezwa na wafugaji ambao hukita kambi ndani ya misitu wakisaka lishe kwa mifugo yao,” alisema.

Baadhi ya wafugaji waliafiki maelezo haya wakisema wamekuwa wakigombania raslimali na wachomaji makaa.

Sehemu kubwa ya msitu iliyochomeka. Picha/ Richard Maosi

“Wakati mwingine vita huzuka pindi maelewano yanapokosekana miongoni mwetu kwa sababu ya uhaba wa nyasi na majani ya miti,” Daniel Ole Kuntai ambaye ni mfugaji alisema.

Anaeleza tangu 2014 amekuwa akifunga safari kutoka kaunti ndogo ya Gilgil, kusaka lishe kwa mifugo wake na hangekubali watu wachache wenye tamaa za kujitajirisha wamfanye ataabike.

Mnamo 2018 Bw Tobiko alihimiza wakenya milioni 45 kupanda miti mitano kila mmoja lakini hilo halijashuhudiwa kufanyika mpaka sasa.

Hili linajiri baada ya wakenya kushuhudia siasa kuingizwa katika swala la kuhifadhi misitu.Kila mara watu walipofurushwa kutoka msituni ilisemekana ni jamii fulani ilikuwa ikilengwa.

You can share this post!

China yazindua apu inayotambua mtu wa madeni akiwa karibu

Nina ushahidi wa kuthibitisha Joho ni mlanguzi wa...

adminleo