Makala

Serikali yakemewa kwa kujenga soko la tatu Ndaragwa ilhali mawili mapya hayatumiki

Na WAIKWA MAINA June 3rd, 2025 Kusoma ni dakika: 1

HATUA ya serikali ya kitaifa kujenga soko kwa kima cha Sh65 milioni karibu na mengine mawili ambayo yalijengwa kwa kima cha Sh35 milioni imewaghadhabisha wakazi wa mji wa Ndaragwa, Kaunti ya Nyandarua.

Mji huo mdogo huenda ukawa na masoko matatu ilhali hata lile lililoko kwa sasa halitumiki japo kwa ujumla Sh100 milioni zimetumikwa kwenye ujenzi wa masoko hayo.

Ujenzi wa masoko mengine mawili umeibua maswali iwapo kweli serikali huthamini mikutano ya ushirikishaji wa umma ambapo  raia hutoa maoni yao kuhusu miradi.

Moja ya masoko haya yalijengwa wakati wa utawala wa Gavana Daniel Waithaka kwa kima cha Sh15 milioni.

Soko la pili lilijengwa na Benki ya Dunia kupitia mpango wa Hazina ya Kimataifa ya Ustawi wa Kilimo (IFAD).  Serikali ya kitaifa sasa inataka kujenga soko la tatu kwa kima cha Sh65 milioni.

Soko lililojengwa kwa kima cha Sh15 milioni Ndaragwa, ambalo halitumiki. Picha|Waikwa Maina

“Mbona soko la tatu lijengwe kwa mji kwa mdogo ambao una masoko mawili ambayo hayatumiki. Kuna masuala mengine mazito na kwa mfano machifu na manaibu chifu wa Muthiga na Nyakinyua hawana ofisi.

“Kule Nyakichua landlodi amemtimua naibu chifu kutoka nyumba ndogo aliyokuwa amekodisha. Wakazi wamelazimika kukusanya fedha zao kumlipia naibu chifu afisi,” akasema Jackson Kahani.

Aliongeza kuwa baadhi ya madarasa kwenye Shule ya Msingi Nyakinyua yako katika hali mbaya na yapo kwenye hatari ya kuporomoka.

Mji wa Ndaragwa nao hauna barabara ya lami, miundomsingi ni mbovu na hakuna mabomba ya kupitisha majitaka.

Naibu Rais Kithure Kindiki akikagua ujenzi wa soko la thamani ya Sh65 milioni Ndaragwa. Ujenzi wa soko hili unafanyika ilhali kuna masoko mengine mawili mapya ambayo hayatumiki, huku kukiwa na uhitaji wa muundomsingi muhimu kama barabara, madarasa na nyumba za machifu. Picha|Waikwa Maina

“Hakuna mkutano unaoshirikisha umma ambao ulifanyika kabla ya soko hilo kuanza kujengwa. Mbona serikali haikushauriana  na raia mwanzoni? Tungewaambia hatuhitaji soko jingine,” akasema Peter Maina mnamo Jumatatu.

Wiki jana, Naibu Rais Profesa Kithure Kindiki akiwa ameandamana na mbunge wa Ndaragwa George Gachagua walikagua ujenzi wa soko ambalo ujenzi wake una thamani ya Sh65 milioni mjini Ndaragwa.