ODM na UDA zapoteza ngome wanasiasa wakijipanga kwa 2027
HATUA ya baadhi ya vyama kujipanga kisiasa kuelekea uchaguzi mkuu wa 2027 imeanza kubadili mwelekeo wa vyama hivyo huku utafiti mpya ukionyesha kuwa umaarufu wa chama cha UDA na mshirika wake katika serikali jumuishi, ODM, umepungua katika baadhi ya maeneo yaliyokuwa ngome zao.
Kulingana na utafiti wa Infotrak uliotolewa Jumatatu, UDA ya Rais William Ruto bado inaongoza kwa umaarufu wa asilimia 22, ikifuatiwa na ODM kwa asilimia 21.
Chama cha Democracy for Citizens Party (DCP) cha aliyekuwa Naibu Rais Rigathi Gachagua kimeorodheshwa cha tatu kwa asilimia tisa.
Jubilee kinaungwa mkono na asilimia sita huku Wiper Democratic Movement cha Kalonzo Musyoka kikipata asilimia tano.
Utafiti huo unaonyesha kuwa, UDA imepoteza pakubwa ushawishi wake katika eneo la Mlima Kenya, ambalo lilikuwa ngome yake kuu wakati wa uchaguzi wa 2022.
Kwa sasa, chama hicho kinaungwa mkono na asilimia tisa pekee katika eneo hilo.
Badala yake, DCP imeibuka kuwa chama maarufu zaidi Mlima Kenya kwa asilimia 33 huku asilimia 36 ya wakazi wakisema bado hawajaamua chama watakachounga mkono.
Katika uchaguzi wa 2022, kaunti 10 za Mlima Kenya pamoja na saba za Bonde la Ufa Kaskazini zilimpa Rais Ruto takriban kura milioni 4.5, sawa na asilimia 63 ya kura zote alizopata.
Hata hivyo, hali hiyo imebadilika kutokana na mivutano ya kisiasa iliyoibuka baada ya kuondolewa mamlakani kwa Bw Gachagua mnamo 2024.
Kwa sasa, UDA inaungwa mkono zaidi Kaskazini Mashariki kwa asilimia 45, Bonde la Ufa kwa asilimia 39 na Pwani kwa asilimia 29.
Magharibi asilimia 18, Mashariki asilimia 16, Nyanza asilimia 13 na Nairobi asilimia nane.
Kwa upande wa ODM, utafiti unaonyesha umaarufu wake umeshuka kutoka asilimia 38 mnamo Septemba 2024 hadi asilimia 21 sasa.
Wachambuzi wanaeleza kuwa ushirikiano kati ya Rais Ruto na kinara wa zamani wa ODM Raila Odinga umechangia mgawanyiko ndani ya chama hicho.
Kutokana na hali hiyo, kundi la Linda Mwananchi linaloongozwa na Seneta wa Nairobi Edwin Sifuna, limeendelea kupata ushawishi kote nchini.