Habari za Kitaifa

Gachagua: Mbunge yeyote wa Mlima anayeshabikia Ruto asubiri kuadhibiwa na raia

Na CHARLES WASONGA June 3rd, 2025 Kusoma ni dakika: 2

ALIYEKUWA Naibu Rais Rigathi Gachagua sasa anadai wabunge wa Mlima Kenya wanaoendelea kuwa waaminifu kwa Rais William Ruto ni “fedheha” kwa eneo hilo.

Akiongea katika Kanisa la AIPCA Gatumbi, eneo bunge la Lari, kaunti ya Kiambu alikohudhuria ibada ya Jumapili, Juni 1, 2025, Bw Gachagua alisema kuwa wabunge kama hao wataadhibiwa vikali na raia debeni 2027.

“Ninyi muendelee tu kusema NDIO kwa William Ruto kinyume na matakwa ya wakazi wa Mlima. Mjue kwamba mtaadhibiwa vikali na wananchi hawa katika uchaguzi mkuu ujao,” akaeleza.

Kwa mara si moja Bw Gachagua amewataka wananchi watowaunga mkono wabunge hao katika uchaguzi mkuu wa 2027 akiwataja kama wasaliti kwa kuunga mkono hoja ya kumtimua afisini mnamo Oktoba 18, 2024 katika Bunge la Kitaifa.

Miongoni mwa wabunge hao ni Kimani Ichung’wah (kiongozi  wa wengi katika bunge la kitaifa), Eric Wamumbi (Mathira), Duncan Mathenge (Njeri Mjini), Anne Muratha (Mwakilishi wa Kike Kiambu), George Gachagua (Ndaragwa), miongoni mwa wengine.

Mnamo Januari mwaka huu, Bw Gachagua alianzisha kampeni kali katika maeneo bunge kadhaa ya Mlima Kenya akiwahimiza wakazi kuwakataa wabunge hao katika uchaguzi mkuu ujao.

Bw Gachagua, ambaye ni Mbunge wa zamani wa Mathira aliwahi kufananisha wabunge, kutoka Mlima Kenya ambao ni wandani wa Rais Ruto, na Waafrika walioshirikiana na wakoloni nyakati za mapambano ya uhuru, maarufu kama “home guards”.

Aliwataja kama wanasiasa wanaohujumu umoja wa Mlima Kenya.

Ujumbe wake umekuwa wazi kwamba: “Wabunge wanaodinda kufuata mkondo wake wa kisiasa wanapasa kukataliwa na wananchi wakati wa uchaguzi mkuu ujao.”

Mnamo Mei 15, 2025 Bw Gachagua alitaja chama Democracy for Citizens Party (DCP) kama chombo cha kisiasa atakachotumia kuhakikisha kuwa anamnyima Rais Ruto kura za Mlima Kenya na kufanikisha lengo lake la kumnyima nafasi ya kuongoza kwa muhula wa pili.

Ameapa kufanikisha ajenda hiyo kwa ushirikiano na vinara wengine wa upinzani kama kiongozi wa Wiper Kalonzo Musyoka, Martha Karua (Peoples Liberation Party), Eugene Wamalwa (DAP-K), aliyekuwa Waziri wa Usalama Fred Matiang’i, miongoni mwa wengine.