Linda Mwananchi ilivyopokonywa jina
VUGUVUGU la Linda Mwananchi limetishia kufanya maandamano ya kila siku nje ya Ofisi ya Msajili wa Vyama vya Kisiasa (ORPP) iwapo ombi lake la kusajiliwa kama chama cha kisiasa halitashughulikiwa.
Hatua hiyo inazidisha mvutano kati ya vuguvugu hilo na ofisi ya Msajili wakati Linda Mwananchi ikijaribu kujibadilisha kuwa chama rasmi cha kisiasa kabla uchaguzi mkuu wa 2027.
Akizungumza wakati wa ziara ya Linda Mwananchi ya kukutana na wananchi katika Kaunti ya Busia siku ya Ijumaa, Seneta wa Vihiga Godfrey Osotsi alilaumu watu ambao hakuwataja kwa kujaribu kunyakua jina linalohusishwa na vuguvugu hilo.
Osotsi alisema kundi hilo litampa Msajili hadi kesho kutatua suala hilo.
Alionya kuwa iwapo suala hilo halitatatuliwa basi wafuasi wa Linda Mwananchi wataanza kufanya mikutano ya kila siku nje ya ofisi za ORPP.
“Ruto ametuma wakora kule kwa ofisi ya msajili wa vyama eti wanajaribu kunyakua hii jina yetu. Mimi nataka kuambia William Ruto, Ibara ya 38 inaruhusu Mkenya yeyote kuunda chama,” alisema Osotsi.
Akaongeza: “Tunaambia huyo msajili kama hutapatiana hiyo jina Jumatatu, tutaandaa mikutano ya kila siku kwa hiyo ofisi.”
Mzozo huo umejikita katika maombi ya kusajili chama na namna Ofisi ya Msajili inashughulikia jina linalopendekezwa na Linda Mwananchi.
Mvutano huo ulipata sura mpya baada ya ORPP kuripotiwa kusajili Liberty National Democratic Alliance, kinachojulikana kama LINDA Party.
Hatua hiyo imeibua mvutano mpya na Seneta wa Nairobi Edwin Sifuna pamoja na washirika wake katika Linda Mwananchi.
Usajili wa chama kinachotumia jina LINDA umeleta changamoto mpya kwa juhudi zao.
Kwa mujibu wa ripoti, chama hicho kipya kinahusishwa na kundi tofauti ambalo pia lilikuwa limejitahidi kupata utambulisho wa kisiasa kwa kutumia jina “Linda”.
Kundi hilo pinzani limepinga madai ya Linda Mwananchi kwamba ndilo lenye haki ya kutumia jina hilo.
Madai hayo yameibua swali kuhusu kundi lenye haki ya kutumia jina na nembo zinazohusishwa na “Linda”.
Mzozo huo pia umewekea Ofisi ya Msajili shinikizo kutoka pande zote.
Viongozi wa Linda Mwananchi wamekuwa wakisisitiza kuwa tayari wamejenga utambulisho wa kisiasa kupitia jina hilo, hivyo wanafaa kupewa nafasi ya kukitumia chama hicho.
Hatua ya hivi majuzi inafuatia mikutano kati ya viongozi wa Linda Mwananchi na Msajili wa Vyama vya Kisiasa John Cox Lorionokou.
Ripoti zinasema kuwa Msajili alikubali kupitia upya uamuzi wa awali wa kukataa jina la Linda Mwananchi baada ya mashauriano na wawakilishi wa vuguvugu hilo.
Hatua hiyo ilikuwa imeibua matumaini miongoni mwa viongozi na wafuasi wa Linda Mwananchi kwamba mchakato wa usajili ungeendelea.
Hata hivyo, usajili ulioripotiwa wa LINDA Party umeleta changamoto mpya na kugubika Linda Mwananchi na mzozo mwingine kuhusu jina inalotaka kutumia.
Wadadisi wanasema haki inayotokana na Kifungu 38 cha Katiba – kinachowapa raia haki ya kuunda au kushiriki katika uundaji wa chama cha kisiasa – inaambatana na masharti ya kisheria yanayosimamia usajili wa vyama vya kisiasa nchini.
Ofisi ya Msajili ina jukumu la kusajili na kudhibiti vyama pamoja na kusimamia taratibu za kisheria zinazohusu kuanzishwa kwa vyama.
Linda Mwananchi sasa inataka ORPP itatue mzozo huo ili iweze kukamilisha miundo yake kabla ya uchaguzi ujao. Usajili wa chama ni hatua muhimu katika kubadilisha vuguvugu hilo kuwa chombo rasmi cha uchaguzi.
Kwa sasa, viongozi wake wameweka Jumatatu kuwa siku ya mwisho kwaMsajili wa Vyama kushughulikia suala hilo kabla kuanza kwa mikutano ya kila siku nje ya ofisi hiyo.