Habari

Wanaharakati wataka Ruto, Museveni, Suluhu wawekewe vikwazo vya kimataifa

Na STEVE OTIENO June 3rd, 2025 Kusoma ni dakika: 2

WANAHARAKATI sasa wanataka vikwazo viwekwe dhidi ya marais wa ukanda wa Afrika Mashariki baada ya wanaharakati Boniface Mwangi na Agatha Atuahire kukamatwa, kuzuiliwa na kuteswa jijini Dar es Salaam mwezi uliopita.

Kwenye taarifa mnamo Jumatatu, makundi ya haki yakiongozwa na Jaji Mkuu Mstaafu wa Kenya Dkt Willy Mutunga walikashifu kutimuliwa kwa wanaharakati Tanzania wakisema ni ukiukaji wa haki zao za kimsingi pamoja na demokrasia.

Pia walizua maswali kuhusu kimya cha marais wa miungano mingine ya kieneo kama ule wa Mataifa Kusini mwa Afrika (SADC) na pia Umoja wa Afrika (AU) pamoja na washirika wao wa kimataifa.

“Tunaamrisha kuwa vikwazo vya kimataifa viwekwe dhidi ya Rais Samia Suluhu wa Tanzania, Yoweri Museveni wa Uganda, William Ruto wa Kenya na mkuu wa majeshi ya Uganda Generali Muhoozi Kainerugaba kwa kuendelea kukandamiza haki na kuwatesa watu wa Afrika Mashariki,” akasema Dkt Mutunga.

Pia makundi hayo yalitoa wito kwa serikali ya Tanzania itoe maelezo ya kina kuhusu kukamatwa, kuzuiliwa na kufurushwa kwa Bw Mwangi na Bi Atuahire.

Wanaharakati hao wawili walikuwa na pasipoti za EAC  na tikiti za ndege wakati wa kufurushwa kwao. Walikuwa kati ya wanaharakati na mawakili ambao walisafiri hadi Dar es Salaam kufuatilia vikao vya kesi dhidi ya Kiongozi wa Upinzani Tundu Lissu mnamo Mei 19.

Bw Mwangi na Bi Atuahire walizuiliwa kwa siku tatu kisha wakafurushwa. Bw Mwangi aliwaachwa kwenye mpaka wa Kenya na Tanzania huku Bi Atuahire akiachwa kwenye mpaka wa Uganda na Tanzania.

Wanaharakati hao sasa wanataka Tume ya Umoja wa Afrika Kuhusu Haki za Kibinadamu kuanza uchunguzi kuhusu dhuluma walizopitia pamoja na nyingine ambazo zimetokea Kenya, Uganda na Tanzania.

“Tunaamrisha kukamatwa kwa maafisa wote wa Tanzania ambao walihusika katika kuwakandamiza wanaharakati.  Pia tunataka uchunguzi ufanywe kuhusu madai ya kuzuiliwa na kudhulumiwa na hilo lifanywe na Tume ya Umoja wa Afrika kuhusu haki katika nchi za Uganda, Kenya na Tanzania,” ikasema taarifa yao ya pamoja.