Siku 1,000 za Ruto: Tathmini yaonyesha umekuwa uongozi wa kubahatisha
RAIS William Ruto aliingia madarakani kwa ahadi nyingi alizowapa raia, akijisawiri kuwa mtetezi wa maskini walio wengi.
Hata hivyo, tathmini ya kipindi cha kati cha utawala wake siku 1,000 baadaye inaonyesha ameshindwa kuzitimiza na kuzua hali ya kutoridhika miongoni mwa umma, ambayo ilifikia kilele mwaka jana wakati wa maandamano dhidi ya ushuru yaliyosababisha umwagaji wa damu.
Alitaja uchaguzi wa urais wa 2022 kama vita kati ya maskini na matajiri na kujipatia umaarufu na hatimaye akaingia Ikulu. Aliahidi kuunda nafasi za kazi kwa mamilioni ya vijana wasio na ajira na kupatia kipaumbele mahitaji ya watu wa kipato cha chini.
Baada ya miaka miwili na nusu madarakani, Wakenya wamegawanyika kuhusu iwapo mwanasiasa huyo aliyekuwa Naibu Rais na sasa Rais ametekeleza ahadi zake za kabla ya uchaguzi.
Wakosoaji wake wamempachika majina ya kejeli kama Zakayo, Kasongo, El Chapo na mengineyo, wakimtania kwa kiu yake ya kuanzisha ushuru zaidi na ahadi zisizotekelezwa.
Katika bajeti yake ya kwanza kwa mwaka wa fedha 2023/2024, serikali ya Kenya Kwanza ilianzisha hatua mpya za ushuru, ikiwemo kuongeza ushuru VAT kwa bidhaa za mafuta kutoka asilimia 8 hadi asilimia 16.
Mapato ya wafanyakazi yalipungua kwa kiasi kikubwa baada ya kuanzishwa kwa makato mapya, ikiwemo asilimia 15 ya ushuru wa nyumba, asilimia 2.7 kwa Hazina ya Bima ya Afya ya Jamii (SHIF) na ongezeko la makato kwa Hazina ya Malipo ya Uzeeni (NSSF).
Hatua nyingine za ushuru katika Mswada wa Fedha wa 2024 zilisababisha maandamano makubwa ya vijana kote nchini, yaliyomlazimu Rais kuondoa mswada huo.
Baadhi ya wandani wake wa zamani katika serikali ya Kenya Kwanza sasa wamegeuka kuwa wakosoaji wake wakuu, wakimlaumu kwa kuharibu uchumi kupitia ushuru wa kikatili.
Hata hivyo, Rais Ruto amekuwa akitoa picha chanya kuhusu mwelekeo wa nchi, akisisitiza kuwa serikali yake bado iko kwenye mkondo wa kuboresha maisha ya wanyonge.
Katika uchaguzi wa 2022, Rais Ruto alijitokeza kama mtetezi wa maskini, Aliahidi kuunda ajira milioni kwa vijana na kuzingatia mahitaji ya wafanyakazi wa kipato cha chini.
Kenya Kwanza iliahidi kujenga nyumba 250,000 kila mwaka na kuongeza upatikanaji wa makazi ya bei nafuu kutoka asilimia 2 hadi 50. Walikusudia kutumia mifumo ya kifedha ya muda mrefu ili kuhakikisha upatikanaji wa nyumba kutoka kwa wastawishaji.
Hata hivyo, baada ya kuingia madarakani, idadi ya nyumba ilipunguzwa kuwa 200,000 kwa mwaka. Mpango huo ulianzisha kodi ya nyumba ya asilimia 1.5 ya mshahara wa kila mwezi wa mfanyakazi na kiasi sawa kutoka kwa waajiri. Kwa sasa, nyumba 148,165 zinajengwa na 11,000 tayari zimekamilika. Huu ni upungufu mkubwa ikilinganishwa na lengo la nyumba 500,000 kufikiaAprili 2025.
Kenya Kwanza iliahidi kutoa Sh50 bilioni kila mwaka kwa wafanyabiashara wadogo kupitia vyama vya Akiba na Mikopo, mitaji ya uwekezaji, na mikopo ya muda mrefu kwa biashara mpya na zinazokua. Hustler Fund ilizinduliwa Novemba 30 2022, na iliahidi kutoa Sh50 bilioni kila mwaka kwa miaka mitano ijayo.
Hata hivyo, Hazina hii imeendelea kupungua kutokana na kutolipwa kwa mikopo. Katika mwaka wa fedha unaoishia Juni 2023, Sh12 bilioni zilitengwa kwa hazina hiyo. Katika mwaka uliofuata unaoishia Juni 2024, Sh800 milioni pekee zilitolewa kwa hazina. Katika mwaka mpya wa kifedha unaoanza Julai 1, imetengewa Sh1 bilioni dhidi ya ombi la Sh5 bilioni.
Kenya Kwanza iliahidi kubadilisha wakulima maskini milioni mbili kuzalisha chakula cha kutosha hadi cha ziada kupitia fedha za pembejeo na msaada wa nyanjani wa kilimo.
Serikali ilitekeleza mpango wa ruzuku ya mbolea na wakulima milioni 53.6 wamesajiliwa. Hata hivyo, mpango wa ruzuku ulijikuta katika kashfa ya rushwa baada ya Naibu Rais wa zamani Rigathi Gachagua kudai kuwa mbolea iliyouzwa kwa wakulima kwa bei nafuu ilikuwa ni msaada kutoka kwa serikali ya Urusi.
Serikali ilianzisha utekelezaji wa bima ya afya ya jamii kupitia Mamlaka ya Huduma ya Afya ya Jamii (SHA). Hata hivyo, mpito kutoka kwa Hazina ya Kitaifa wa Bima ya Afya (NHIF) umeambatana na changamoto kubwa za utekelezaji. Licha ya kulipa michango ya kila mwezi, wagonjwa hawawezi kupata matibabu kwa wakati kutokana na kufeli kwa mifumo.
Ripoti ya Chama cha Hospitali za Kibinafsi (RUPHA) ilionyesha kuwa taasisi tisa kati ya kumi za umma na binafsi zinakabiliwa na changamoto za kukidhi gharama zao kutokana na kuchelewa kwa malipo kutoka SHA.
Kenya Kwanza iliahidi kuziba pengo la uhaba wa walimu 116,000 ndani ya miaka miwili ya kifedha. Waliahidi pia kuboresha uwezo wa shule za sekondari za kutwa ili kuhakikisha upatikanaji wa elimu bora na kupunguza gharama ya elimu.
Hata hivyo, serikali imekuwa ikikumbwa na changamoto za kifedha katika kugharamia elimu katika shule za umma. Waziri wa Elimu Julius Migos aliambia wabunge kuwa serikali inadaiwa na shule Sh64 bilioni.
Rais Ruto alijitokeza kama kiongozi wa wanyonge, akiahidi kupunguza gharama ya maisha. Hata hivyo, bajeti yake ya kwanza Julai 1, 2023 ilifanya maisha kuwa magumu zaidi huku biashara zikitozwa ushuru mkubwa. Serikali iliongeza VAT kutoka asilimia 8 hadi 16 kwa bidhaa za mafuta, na hii iliongeza gharama ya maisha, ikiwa ni pamoja na bei ya bidhaa za msingi kama unga wa mahindi na mkate.
Gavana wa Benki Kuu ya Kenya (CBK) Kamau Thugge alisema uchumi wa nchi ulipata shinikizo kubwa la mfumuko wa bei na mabadiliko ya viwango vya kubadilisha fedha mwaka 2022, hasa kutokana na kuongezeka kwa bei za kawi na chakula duniani.
Serikali ya Kenya Kwanza iliahidi kufanya kuwa dijitali asilimia 80 ya huduma za serikali kwa lengo la kuboresha ufanisi, kupunguza rushwa, na kuongeza upatikanaji kupitia eCitizen na majukwaa ya simu.
Idadi ya huduma za serikali zilizotolewa kidijitali imeongezeka kutoka 350 mwaka 2022 hadi 20,985 mwaka 2025. Dijitali, serikali ilisema, imeongeza ukusanyaji wa mapato kutoka Sh60 milioni hadi kati ya Sh700 milioni na Sh1 bilioni kwa siku.
Rais Ruto alijitolea kupambana na ufisadi. ‘Nikipata fursa ya kuendesha serikali, hakutakuwa na ufisadi kwa sababu hakutakuwa na pesa ya kuiba kwani kila senti itatumika. Hakutakuwa na senti inayozunguka mahali popote kwa mtu kuiba,’ aliahidi Rais Ruto.
Hata hivyo, mwaka mmoja baada ya kuingia madarakani, kashfa kadhaa zimetikisa serikali ya Kenya Kwanza, ikiwa ni pamoja na zabuni ya vyandarua ya Mamlaka ya Usambazaji wa Dawa na Vifaa vya Matibabu Kenya (Kemsa) ambapo mamilioni ya pesa ziliporwa na maafisa wa serikali wasio waaminifu.
Ripoti ya Tume ya Huduma za Umma (PSC), mwaka wa kifedha wa kwanza wa utawala wake, ilionyesha kuwa serikali ilipoteza Sh650 milioni kupitia mikataba ya rushwa katika kipindi kilichofanyiwa ukaguzi.