Wazee waonya mwenzao, 78, aliyeiga mbwembwe za Gen-Z
BARAZA la wazee kijijini hapa lililazimika kuandaa kikao cha dharura kuonya mmoja wa wanachama wake.
Hii ni baada ya tabia, lugha, mavazi na mienendo ya mzee huyo wa miaka 78 kubadilika ghafla.
Hivi majuzi mzee huyo alimtembelea mmoja wa watoto wake wanaoishi mjini.
Inaaminika mitindo ya mavazi na muonekano wa vijana wanaoishi jijini ndiyo iliyomgeuza mzee kimtazamo kwani tangu arudi amekuwa akivalia mavazi ya kizazi cha Gen Z.
Ni hali ambayo imemwacha mkewe, watoto, wajukuu na hata majirani ambao wamekuwa wakiishi naye mashambani kumshangaa na hata kuhisi kuaibika.
Juhudi za mkewe kujaribu kumweleza aache kuiga mtindo wa vijana ziligonga mwamba kwani amekuwa akidakia kwamba yeye bado ni mdogo.
“Sikiliza wewe. Mimi bado natamba. Uniache kabisa,” akafoka buda huyo naye akafahamisha baraza la wazee mtaani mzee akaitwa kushauriwa akome kuiga rika ambalo halilingani na umri wake uliosonga.