Makala

Kindiki, Kalonzo waumbuana wakiwania kura za Ukambani

Na KITAVI MUTUA June 17th, 2025 Kusoma ni dakika: 2

UBABE wa kisiasa umeibuka kati ya Naibu Rais Profesa Kithure Kindiki na Kinara wa Wiper Kalonzo Musyoka huku kura za eneo la Ukambani zikilengwa mnamo 2027.

Wiki jana, Profesa Kindiki alimrai Bw Musyoka abadili nia na ajiunge na Serikali Jumuishi inayoongozwa na Rais William Ruto na Kinara wa Upinzani, Raila Odinga.

Hata hivyo, Bw Musyoka ameweka wazi kuwa hatawatema wandani wake wa upinzani na kujiunga na serikali.

Profesa Kindiki naye amemkashifu kwa kuendeleza madai ya uongo ili kupaka tope uongozi wa Kenya Kwanza. Profesa Kindiki alikasirishwa na kauli ya Bw Musyoka kuwa utawala wa Kenya Kwanza una damu kwenye mkono wake.

Pia alishangaa kwa nini Profesa Kindiki hajaomba Gen Z radhi kutokana na mauaji yaliyotokea mwaka jana wakati ambapo alikuwa Waziri wa Usalama wa Ndani.

Wiki jana, Profesa Kindiki alikuwa amepiga kambi eneo la Ukambani kwa zaidi ya siku 10 huku akishiriki michango ya kuyainua makundi ya vijana na akina mama na akawaomba wakazi wa eneo hilo waasi upinzani na kujiunga na serikali.

Hata hivyo, Bw Musyoka alionekana kumjibu Profesa Kindiki kimadharau akisema aliteuliwa kuwa naibu rais kwa nusu muhula katika serikali itakayohudumu kwa muhula moja pekee.

“Sina tatizo lolote na ndugu yangu mdogo Profesa Kindiki lakini nina shida na Rais William Ruto ambaye ameharibu nchi hii na nani anajua, huenda nitakuwa kwenye debe kama mpinzani wake,” akasema Bw Musyoka akimtaka Profesa Kindiki akome kutumia jina lake visivyo.

Kinara huyo wa Wiper alikariri kuwa upinzani utaendelea kuungana kuhakikisha Rais Ruto anapoteza kura mnamo 2027 lakini kwa njia ya demokrasia.

“Wanaweza kuruka kutoka juu hadi chini na hilo halitakuwa na maana yoyote. Hatutakomesha shinikizo au kuinua mkono wala hatutanunuliwa au kulazimishwa kuungana na serikali,

“Wiki ijayo tutaandaa maombi ya kuadhimisha mwaka moja kama kumbukumbu kwa Gen Z ambao waliuawa mwaka jana,” akasema Bw Musyoka mnamo Jumapili akiwahutubia waumini wa Kanisa la Salvation Army, Ngong, Kaunti ya Kajiado.

Vilevile Bw Musyoka alizua maswali kuhusu marufuku aliyoiweka Rais Ruto kwenye harambee ilhali naibu wake amekuwa akizunguka kotekote na pesa za walipa ushuru akishiriki michango kwa makundi mbalimbali ilhali ana lengo la kisiasa.

Alidai pesa anazotoa Profesa Kindiki na viongozi wengine kwenye michango ni ya kuwahonga Wakenya ili wawapigie kura mnamo 2027.

Akimjibu, Profesa Kindiki alisema hana tatizo iwapo Bw Musyoka amekataa kufanya kazi naye lakini akamkashifu kwa kueneza uongo kumhusu.

“Kuhusu mabaya amesema juu yangu, sitamjibu hadharani kwa sababu huwa sishiriki ugomvi na watu ambao nawaheshimu,” akasema Profesa Kindiki.

Hata hivyo, alisema hatasita kumkabili uso kwa macho akiendelea kueneza uongo kumhusu. Wiki jana, naibu rais alizuru kaunti zote za Ukambani akishiriki michango ambako alitoa wito eneo hilo lisikubalie kusalia kwenye upinzani.