Gikaria matatani kwa madai ya kutoa hongo Ol Kalou akipigia debe mwaniaji wa UDA
MBUNGE wa Embakasi Mashariki David Gikaria alipewa hadi saa saba unusu kufika mbele ya Kamati ya Maadili na Nidhamu ya Tume Huru ya Uchaguzi na Mipaka Nchini (IEBC) baada ya kukosa kufanya hivyo licha ya kuitwa hapo awali.
Kamati hiyo inayoongozwa na Dkt Alutalala Mukhwana ilisitisha shughuli zake baada ya mbunge huyo kumtuma msaidizi wake Joseph Kariuki Nelima kumwakilisha katika kikao hicho.
Kwenye uamuzi wake, Dkt Mukhwana alisema hawakuridhishwa na sababu zilizotolewa na msaidizi huyo kuhusu kutofika kwa Bw Gikaria.
“Hatujaridhishwa na sababu zake kuhusu kutofika kikaoni kuhusu suala hili. Kwa hivyo, tunasitisha shughuli za kamati hii ili kumpa Bw Gikaria nafasi ya kusikizwa,” akasema Dkt Mukhwana.
Bw Gikaria anakabiliwa na dai la kukiuka mwongozo wa IEBC kuhusu uchaguzi mdogo.
Inadaiwa alishiriki utoaji hongo kwa wapigakura alipokuwa akimfanyia kampeni mgombeaji wa UDA Samuel Muchina Nyaga.
Kupitia msaidizi wake wa kibinafsi, Bw Gikaria aliambia kamati hiyo kwamba alikuwa mgonjwa na ni sadfa alitakiwa kufika mbele ya kamati wakati ambapo alikuwa amwone daktari wake.
Mbunge huyo pia alidai kuwa hakuwasilishiwa malalamishi dhidi yake kwa njia inayofaa akisema alifahamu suala hilo kupitia mtandao wa kijamii.
“IEBC inafaa kufuata sheria. Mimi ni mgonjwa na nina miadi na daktari,” akasema Bw Gikaria.