Kivuti amlima Ruto katika hotuba ya kujiunga na upande wa Gachagua
KWA mara ya kwanza kabisa, aliyekuwa Seneta wa Embu Lenny Kivuti amefichua jinsi alivyokataa pendekezo la Rais William Ruto la kumteua kuwa Waziri wa Utumishi wa Umma kufuatia kufutwa kwa Bw Justin Muturi.
Ameelezea sababu iliyochangia uamuzi wake kukataa uteuzi huo.
“Rais alinipigia simu na kuniambia alitaka kunipa kazi. Nikajibu kwamba ningeshukuru mradi kazi hiyo si ile ya Muturi,” Bw Kivuti akasema.
Seneta huyo wa zamani wa Embu, alimwomba Rais Ruto amtunukie wadhifa mwingine tofauti na ule alioushikilia Bw Muturi.
Ni hapo ambapo Dkt Ruto alimwambia kwamba kazi ya Waziri wa Utumishi wa Umma ndiyo iliyokuwepo na kwamba alipaswa kuikubali.
Bw Kivuti, ambaye pia ndiye Mwenyekiti wa Kitaifa wa Chama cha Devolution Empowerment Party (DEP) alieleza kuwa Muturi alikuwa rafiki yake wa karibu na asingechukua wadhifa wake.
“Nilikataa pendekezo hilo na kuamua kwamba nitaendelea kufanyakazi na Bw Muturi ambaye ni kiongozi wa chama cha Democratic Party (DP),” akaeleza Bw Kivuti.
Kulingana na mwanasiasa huyo, kile ambacho Dkt Ruto alifanya ilikuwa sawa na kumvua mavazi Bw Muturi na “kumwacha uchi”.
Bw Kivuti jana alisema chama cha DEP kitaunga mkono mgombea wa DP katika uchaguzi mdogo wa kuwania kiti cha ubunge cha Mbeere Kaskazini.
“Tumeamua kwamba baada ya Muturi kupoteza nafasi ya uwaziri, tunapaswa kuunga mkono chama chake ili kishinde katika uchaguzi mdogo ikizingatiwa kuwa kiti hicho kilikuwa chake, kikishikiliwa na Geoffrey Ruku,” akasema Bw Kivuti.
Alimshutumu Bw Ruku kwa kukubali wadhifa wa Waziri wa Utumishi wa Umma baada ya kutimuliwa kwa Bw Muturi.
“Baada ya Ruku kupata habari kuhusu kufutwa kazi kwa Muturi, alikimbia kumuona Rais. Alipelekwa Ikulu na mwanasiasa wa cheo cha juu ambaye ni mfuasi sugu wa serikali ya Kenya Kwanza. Ruku alikosea kwa kumsaliti Muturi,” akasema Bw Kivuti.
Alisema chama cha DEP kimejiunga rasmi na kambi ya kisiasa ya aliyekuwa Naibu Rais Rigathi Gachagua ili “kuikomboa nchi hii kutokana na uongozi mbaya.”
Bw Kivuti alikuwa akiongea Jumatatu jioni wakati wa Kongamano la Kitaifa la chama cha DEP mjini Embu.
Mwanasiasa huyo alisema serikali ya Rais Ruto imepoteza umaarufu na hawataki kujihusisha nayo.
“Tumeamua kusikiza matakwa ya watu mashinani na kutekeleza matarajio yao,” akasema Bw Kivuti.
Wajumbe wa DEP waliapa kufuata mkondo wa kisiasa unaofuatwa na Wakenya wengi.
“Tumeamua kuunganisha DEP na vuguvugu lililoanzishwa na binamu zetu lakini bila kuvunja chama chetu na kujiunga na chama chochote. Hatutaki kufanya kosa, tunataka kuelekea mahala Wakenya wako. Kwa hivyo, tutadanyakazi na Gachagua, Kalonzo Musyoka, Eugene Wamalwa, Uhuru Kenyatta, Justin Muturi, George Natembeya na Martha Karua ili tuikomboe nchini hii kutoka kwa utawala dhalimu,” akaeleza Bw Kivuti.