‘Afghanistan’ ya Kaunti ya Homa Bay yaanikwa kwa kusheheni vumbi na uchakavu
MKUTANO wa kisiasa wa Linda Mwananchi uliofanyika Homa Bay Jumapili ulifichua upande wa kaunti hiyo ambao Wakenya wengi huwa hawauoni.
Picha za Homa Bay zinapowekwa mtandaoni, mara nyingi huonyesha fukwe za mchanga, vilima vya kijani, Ziwa Victoria na wanyamapori katika Mbuga ya Kitaifa ya Ruma.
Lakini mbali na mandhari hayo kuna Homa Bay nyingine ambayo wakazi wanaijua vyema na hii ni barabara inayounganisha Kituo cha Biashara cha Kiabuya na ufuo wa Nyandiwa.
Wakenya walipokuwa wakifuatilia mkutano huo kupitia simu, hawakusikiliza hotuba pekee bali pia walitazama mandhari katika maeneo yaliyotembelewa na Gavana James Orengo, Seneta Edwin Sifuna na Mbunge wa Embakasi Mashariki Babu Owino.
Barabara ya Nyandiwa, ambako mkutano wa kwanza ulifanyika, ilivutia zaidi kutokana na hali yake ya vumbi na uchakavu. Baadhi ya watumiaji wa mitandao ya kijamii waliifananisha kwa kejeli na Afghanistan na Gaza.
Picha kutoka video za moja kwa moja zilionyesha barabara za Suba Kusini ikiwa katika hali mbaya, huku baadhi ya maeneo yakiwa bila nguzo za umeme.
Vilevile, picha moja ilionyesha Ziwa Victoria kwa mbali, huku mandhari yakiwa kame na bila miti mingi. Baadhi ya watumiaji waliita eneo hilo kwa mzaha “Mwanzo wa Hormuz”.
Hata hivyo, wengine walisema hali ya barabara ni ushahidi wa miaka mingi ya kutengwa kwa eneo hilo na serikali zilizopita.
Mbunge wa Suba Kaskazini, Millie Odhiambo, alikiri kuwa barabara nyingi eneo la Suba Kaskazini na Suba Kusini ziko katika hali mbaya.
Bi Odhiambo alisema serikali ya Rais William Ruto imeweka lami kwenye Barabara ya Mzunguko ya Rusinga na kufungua Barabara ya Mzunguko ya Mfangano, huku Sindo-Mbito ikiwa miongoni mwa barabara nyingine zilizopangiwa kufanyiwa kazi.
Gavana Gladys Wanga alisema kutengwa kwa eneo hilo kwa kiasi fulani kulitokana na ODM kuwa chama cha upinzani kwa miaka mingi.
“Tuache kuwapotosha watu kwa kusema hizi ni barabara za mashambani na kwamba barabara kuu zilikuwa zimezuiwa. Unachoona hapa, isipokuwa barabara ya Homa Bay hadi Mbita na Barabara ya Mzunguko ya Rusinga, ni barabara kuu. Rais Kibaki na Waziri Mkuu Raila waliweka lami barabara ya Homa Bay hadi Mbita. Rais Uhuru Kenyatta alijenga daraja la Mbita,” akaandika kwenye ukurasa wa Facebook.
Aliahidi barabara hiyo ingekarabatiwa.
“Sasa tuko ndani ya Serikali Jumuishi, na barabara ya Suba itakarabatiwa chini ya mradi wa Barabara ya Mzunguko ya Ziwa Victoria. Waziri Mbadi ametia saini ili kuhakikisha inaboreshwa,” akasema.
Bw Sifuna alishangaa kwa nini barabara hiyo ilikuwa katika hali mbaya ilhali iko karibu na nyumbani kwa Waziri wa Fedha John Mbadi.
“Juzi tuliambiwa kwamba kwa sababu mnaunga mkono Serikali Jumuishi, barabara zote zimewekewa lami. Leo tumekula vumbi. Tumekula vumbi sawasawa,” akasema.
Alisema kwamba wakazi wa Homa Bay bado hawajanufaika kikamilifu na miradi ya serikali kuu.
“Hakuna tofauti kati yenu na sisi Magharibi. Bado mnasafiri kwenye barabara za vumbi kama sisi,” alisema.
Baadhi ya picha zilizotengenezwa kwa AI pia zilisambaa mtandaoni, lakini Taifa Leo ilithibitisha kuwa barabara iliyoonyeshwa ni njia inayotumiwa kwa kawaida na wenye magari kutoka Kiabuya hadi Nyandiwa.
Katika sehemu moja, magari hulazimika kuvuka kijito, huku magari yenye injini dhaifu yakitatizika kupanda mteremko mara baada ya kuvuka.