Habari

Fedheha mji wa Bomet ukikosa maji miezi 8 kwa deni la Sh18 milioni

Na VITALIS KIMUTAI June 22nd, 2025 Kusoma ni dakika: 1

KWA miezi minane sasa, wakazi wa mji wa Bomet wamekuwa wakikumbwa na uhaba mkubwa wa maji kutokana na kukatwa kwa umeme katika mitambo ya kusambaza maji, kufuatia deni la takriban Sh18 milioni ambalo halijalipwa.

Maji hayapatikani hata katika afisi ya Gavana, makao makuu ya kaunti, ofisi za kitaifa na kaunti, makazi ya binafsi na katikabiashara, hoteli na taasisi mbalimbali.

Kampuni ya Maji na Usafi ya Bomet (Bomwasco), inayomilikiwa na serikali ya kaunti, haina uwezo wa kusambaza maji baada ya umeme kukatwa kutokana na deni hilo la karibu Sh20 milioni.

Kwa sasa, kampuni hiyo inatumia malori ya kubeba maji kupeleka maji ofisi muhimu huku wachuuzi wa maji wakivuna pakubwa kwa kuuzia wakazi maji wakitumia pikipiki na malori.

“Tunauza lita 20 za maji kwa Sh20, lakini mahitaji ni makubwa sana kiasi kwamba hatuwezi kuwahudumia wote,” alisema Bw David Langat, mchuuzi wa maji mjini Bomet.

Serikali ya kaunti tayari imelipa Sh10 milioni na kuahidi kulipa Sh8 milioni zaidi kabla ya mwisho wa mwezi ili huduma za umeme zirudishwe na usambazaji wa maji uanze tena.

Gavana Hillary Barchok amekiri kuwa serikali yake inakumbwa na changamoto kubwa ya kugharamia usambazaji wa maji kutokana na gharama ya juu ya umeme.

“Kenya Power wamejumuisha bili zote za vituo vyote vya maji. Hata tukilipa sehemu moja, hawawezi kurejesha umeme hadi tukamilishe deni lote. Tupo kwenye harakati za kutafuta suluhisho la kudumu,” alisema Profesa Barchok.

Hata hivyo, gavana huyo alisema kwamba kukamilika kwa mradi wa maji wa Bomet-Longisa-Mulot wa thamani ya Sh1.2 bilioni, unaofadhiliwa na Benki ya Maendeleo ya Afrika (AfDB), utasaidia kupunguza uhaba wa maji.

Mradi huo unasambaza maji kwa njia ya mvuto na hivyo hautategemea umeme.