Machungu ya walimu wakikosa kupandishwa vyeo
KAZI ya ualimu imegeuka tamu chungu kwa maelfu ya walimu ambao wamekwama kwenye daraja moja kwa miaka mingi huku wakilazimika kushuhudia walimu wenzao wachanga wakiwapita na kupandishwa vyeo.
Licha ya kutumia hela nyingi kujiendeleza kielimu, kutuma maombi ya kupandishwa vyeo mara kadhaa na kuitwa kuhojiwa, idadi kubwa ya walimu wamebaki na machungu dhidi ya mfumo wanaohisi umewasaliti.
Kulingana na alama za TSC, kiwango cha chini zaidi ni B5 na cha juu zaidi ni D5.
Gredi b5 ni kiwango cha kuingilia huduma ya kufunza katika shule ya msingi kinachofuatiwa na C1 (mwalimu wa shule ya msingi), C2 (mwalimu wa kiwango cha juu II), C3 (mwalimu wa kiwango cha juu I), C4 (naibu mwalimu mkuu II) na C5 (mwalimu mkuu).
Kisha kulingana na daraja ya walimu wakuu kuna D1 (mwalimu mkuu wa kiwango cha juu) D2 (naibu mwalimu mkuu II), D3 (mwalimu mkuu), D4(mwalimu mkuu wa daraja ya juu) na D5 (mkuu wa walimu wakuu).
Mwalimu kutoka Nakuru kwa jina Simon Karanja aliye katika daraja la C2 alisimulia kuhusu taaluma yake ambayo imemwacha na machungu na majuto chungunzima.
Huku akiwa amebakisha mwaka mmoja tu astaafu, alisimulia safari yake katika TSC ambayo haijamwachia sababu yoyote ya kutabasamu.
“Nimekwamba katika kiwango cha P1 kwa miaka 27, licha ya kuhudhuria mahojiano tele ambapo nilipokea barua baada ya nyingine za kukataliwa,” anaeleza.
“Ni baada ya tu ya kuandikia barua afisi ya Malalamishi ya Umma, Spika wa Bunge la Kitaifa, Wakili Mkuu, na hata rais, ambapo kitu kilisonga.”
“Afisi ya Malalamishi ya Umma ilijibu na punde baadaye nikapandishwa cheo. Lakini maji yalishamwagika.”
Akiwa mwaka wake wa tatu katika Daraja la Kazi C2, Bw Karanja anasema amepoteza imani na haki katika TSC na kuamini kwamba sehemu kubwa ya kupandishwa cheo husukumwa kisiasa.
Hisia zake zimekaririwa na wengine wengi kote nchini akiwemo Naibu Mwalimu Mkuu wa Shule ya Msinyi ya Kayole, Dismus Omollo, ambaye amekwama katika Daraja la Kazi C4 kwa miaka 19 (tangu 2006) licha ya kutuma maombi ya kupandishwa cheo mara tatu.
Bi Berline Langat, mwalimu wa C1 jijini Nairobi amekwama katika kiwango hicho hicho tangu 2014 (miaka 11) huku kusahihisha kila siku vitabu vya wanafunzi 80 katika kipindi cha dakika 35 kukimlemea kimwili na kihisia.
Bi Florence Wanjiru ambaye amekwama katika Daraja la Kazi c2 tangu 2015 (miaka 10) anasema ualimu ni taaluma ya kujitolea mhanga bila kuzawadiwa, baada ya kuhojiwa mara tatu pasipo mafanikio.
Hisia zake zinarejelewa na Lenah Chebet, mwalimu kutoka Bomet akisema “nilijiunga na huduma hii 2010, nikakwama B5 hadi 2020 (miaka 10) ambapo katika shughuli ya kuwapandisha vyeo walimu wote kwa jumla nilipanda C1 na kukwama hapo hadi leo hii.”