Habari za Kitaifa

Kalonzo, Karua, Maraga na Wamalwa wajiunga na maandamano, waelekea majengo ya Bunge

Na BENSON MATHEKA June 25th, 2026 Kusoma ni dakika: 1

Viongozi wa upinzani wamejitokeza katikati mwa jiji la Nairobi kuungana na familia za waathiriwa wa maandamano ya Gen Z  miaka ya 2024 na 2025.

Kiongozi wa Wiper, Kalonzo Musyoka, kiongozi wa PLP Martha Karua, aliyekuwa Jaji Mkuu David Maraga na kiongozi wa DAP-K Eugene Wamalwa walijiunga na familia za waliouawa katika maandamano ya kupinga Mswada wa Fedha wa 2024.

Kundi hilo linatembea kuelekea majengo ya Bunge kuweka shada za maua kwa heshima ya vijana waliopoteza maisha wakati wa maandamano hayo yaliyotikisa taifa mwaka jana.

Bi Karua alisema hana matarajio ya kushuhudia uporaji au uharibifu wa mali wakati wa maandamano ya mwaka huu kutokana na vizuizi vingi vya polisi vilivyowekwa katika barabara zinazoelekea katikati mwa jiji.

“Kwa vizuizi vyote vilivyowekwa na polisi, hatutarajii kuona wahuni wakitumia maandamano haya kufanya uporaji au kusababisha fujo,” alisema.

Kwa upande wake, Bw Musyoka alisema wito wa kukaa nyumbani uliotolewa na waandalizi wa maadhimisho hayo umefanikiwa kwa kiasi kikubwa.

“Biashara nyingi zimefungwa katika Nairobi na matatu haziruhusiwi kuingia jijini. Hii inaonyesha kwamba wananchi wameitikia wito huu,” alisema.

Viongozi hao wanasisitiza kuwa shughuli zao zinalenga kuwakumbuka waliopoteza maisha na kuhimiza uwajibikaji wa serikali pamoja na kuheshimiwa kwa haki za wananchi.