Guyo apata afueni kuhusu kutimuliwa kwake
GAVANA wa Isiolo, Abdi Guyo, amepata afueni baada ya Mahakama Kuu ya Meru kudumisha amri ya awali iliyozuia Bunge la Kaunti kuendeleza kumfurusha.
Gavana Guyo alitimuliwa Alhamisi baada ya madiwani 16 waliokuwepo kupitisha mswada uliowasilishwa na Diwani wa Kericho, Abubakar Godana.
Hata hivyo, Jaji Heston Mbogo, kupitia korti ya kimtandao alisema amri iliyotolewa Juni 23 ingali inatumika na hatua yoyote iliyochukuliwa na bunge la kaunti ilikiuka agizo la mahakama.
“Maagizo yaliyotolewa Juni 25, 2025 yangalipo. Vitendo vyovyote vya washtakiwa au kundi lingine lolote, vinavyokaidi amri ya korti, havina mashiko. Maagizo yatazidi kutumika hadi korti itakapoyafutilia mbali,” alisema Jaji Mbogo.
Wakili Ekuru Aukot aliyewaakilisha washtakiwa, alieleza mahakama kuwa watakata rufaa kuhusu uamuzi huo mara moja.
Bw Abdi Hassan aliwasilisha kesi na kupatiwa amri ya korti dhidi ya bunge la kaunti, spika na karani kuhusu mswada wa kumtimua Juni 18.
Jana, mawakili wa Bw Hassan ambao ni Eric Theuri na Elias Mutuma, waliwasilisha kesi ya kukaidi amri ya korti dhidi ya Spika na Karani.
Jaji Mbogo aliwaagiza Spika na Karani kufika binafsi kortini Jumatatu, wiki ijayo, kujibu madai ya kukaidi amri ya mahakama.
Hii ni baada ya timu ya mawakili wao, Dkt Aukot, mabwana Paul Wafula, Alex Mbaya na Boniface Mwereru, kuepuka kujibu ikiwa bunge la kaunti limezingatia amri ya korti.