Matiangí: Ruto hanitishii, nitavua koti na kumkabili
ALIYEKUWA Waziri wa Usalama wa Ndani Fred Matiang’i Ijumaa, Juni 27,2025 alieleza matumaini yake kuwa atakitwaa kiti cha urais katika uchaguzi mkuu wa 2027.
Dkt Matiang’i pia amedokeza kuwa hivi karibuni ataanza msururu wa shughuli za kisiasa zinazolenga kuimarisha umaarufu wake ili amng’oe Rais William Ruto mamlakani.
Akizungumza alipohudhuria mazishi ya eneobunge la Bomachoge Chache, Kaunti ya Kisii mnamo Ijumaa, Waziri huyo wa zamani alisema Kenya inaelekea pabaya kwa sababu ya kuongezeka kwa mauaji ya wale wanaodhaniwa kukosoa utawala wa Kenya Kwanza na ongezeko la gharama ya maisha.
“Tuiombee nchi yetu kwa sababu kama mnavyoona, mambo si mazuri, tumefikia wakati mgumu. Mliona yale yaliyotokea juzi watoto wetu walipouawa lakini wale walioko madarakani wanadai kuwa wauaji wao walitoka katika jamii moja.
Niwaulize nyinyi watu wangu, hamjaona kwamba nchi inaelekea pabaya? Sasa ni wakati wa kuangalia jinsi gani tunaweza kuijenga upya nchi yetu kwa sababu kama mambo yalivyo, tutaangamia,” Dkt Matiang’i alisema huku halaiki ya waombolezaji wakimshangilia.
“Tumeanza safari, Tumejiandaa vyema na tutasafiri safari hii pamoja hadi tutakapoingia katika nyumba hiyo (Ikulu). Niko tayari. Na hivi karibuni nitavua koti langu na kuwakabili uso kwa macho,” akaongeza.
Waziri huyo aliyekuwa na usemi mkubwa wakati wa enzi za utawala za rais mstaafu Uhuru Kenyatta, aliwakashifu wakosoaji wake ambao wamekuwa wakimwita mwoga na kumwambia Rais Ruto ajitayarishe kwa kinyang’anyirio kikali katika uchaguzi mkuu ujao.
“Mnanijua vyema na hakuna mtu anayeweza kunitisha. Hatuwezi kukaa wala kutazama watu wengine wakiharibu nchi yetu huku sisi tukisalia pembeni. Lazima pia tuinuke na kusimama kuhesabiwa katika uongozi wa taifa hili,” akasema Dk Matiang’i. .
Alitoa wito kwa viongozi wote waliochaguliwa katika jamii ya Gusii kusalia nyuma nyuma yake, akisema sasa ni wakati wa jamii kuzungumza kwa sauti moja.
Dkt Matiang’i alisema tangu atangaze azma yake ya urais mwezi Mei, wakati alikaribishwa nyumbani kwa kishindo kikuu, amekuwa akishirikiana na viongozi wengine wa upinzani kuhusu jinsi wanavyoweza kukomboa taifa. Mbunge wa eneo hilo Alfah Miruka, ambaye alikuwa miongoni mwa viongozi wengine walioungana na Dkt Matiang’i kuhudhuria mazishi hayo alizomewa na waombolezaji.
Bw Miruka, ambaye ni mbunge wa UDA ni mshirika wa karibu wa Rais Ruto na ni miongoni mwa viongozi wachache kutoka eneo la Gusii ambao wamekuwa wakimpinga Dkt Matiang’i.
Mara tu aliposimama kuzungumza, Bw Miruka alipokelewa na nyimbo za kumpinga Rais Ruto huku baadhi ya vijana wakimshtumu kwa kile walisema ni “kusaliti” jamii.
Bw Miruka alijaribu kusisitiza kwamba aruhusiwe kuhutubia waombolezaji lakini vijana walipungia mkono kwa pamoja kwamba hawakutaka kumsikiliza. Sherehe ya maziko ilikamilika bila Bw Miruka kuhutubia waombolezaji katika ngome yake.
Seneta wa Kisii Richard Onyonka, wabunge Innocent Obiri (Bobasi), Obadiah Barongo (Bomachoge Borabu), Anthony Kibagendi (Kitutu Chache Kusini) na Naibu Gavana Elijah Obebo pia walihudhuria.
Wote waliapa kumuunga mkono Dkt Matiang’i. Hii ilikuwa mara ya kwanza kwa Dkt Matiang’i kurejea hadharani katika ngome yake ya Gusii kufuatia tangazo lake kwamba atawania kiti cha urais mwezi Mei.