Wakazi waibua wasiwasi kuhusu magenge; polisi wasema wako chonjo
WAKAZI na viongozi kutoka ukanda wa Pwani wameendelea kuibua hisia kali kutokana na visa vya kuhangaishwa na magenge ya vijana wanaojihami kwa mapanga, ambao kila baada ya muda huwavamia, kuwaibia na hata kuwajeruhi, licha ya polisi kusema wako chonjo.
Katika kisa kilichotokea Januari 28, kilichoibua minong’ono na kukaripiwa vikali na mbunge wa Nyali Mohammed Ali, video iliyonaswa na kamera za siri ilionyesha vijana hao wakimhangaisha mwanabiashara eneo la Mtwapa.
Licha ya kujaribu kutetea mali yake vijana hao waliingia wakampiga na kumjeruhi, wakamwacha akivuja damu huku akiomba usaidizi.
Vijana hao zaidi ya tano walijifanya kuwa wanunuzi nje ya duka, kabla ya kujaribu kuvunja lango kwani muuza duka huyo alikuwa ashafunga duka na alikuwa akiuzia kwenye vishimo vidogo vilivyokuwa kwenye lango la duka.
“Ongezeko la utovu wa usalama katika eneo la Pwani haswa Kilifi na Mombasa linatisha kwani wizi umekuwa jambo la kawaida. Idara ya polisi inapaswa kuchukua hatua. Isitoshe inapaswa kutafuta suluhisho la kudumu kwa kuwa watu wetu wanahitaji kuishi kwa amani na siyo kwa uoga,” akasema Bw Ali.
Kwa muda mrefu suala la magenge yanayowahangaisha Wapwani na Wakenya kwa ujumla lilikuwa limezungumziwa kwa muda, serikali kupitia idara ya wizara ya ndani ikiahidi kujitolea kukabiliana na hata kutafuta njia za kuwarekebisha vijana wanaojisalimisha.
Kwa mujibu wa Mbunge huyo juhudi zilizokuwa zikitiwa na polisi kukabiliana na magenge hayo hayakuwa ya kutosha, kwa kuwa visa hivyo vilikuwa vikijirudia rudia baada ya muda.
Malalamishi ya Wakenya yaliisukuma idara ya polisi, kuchunguza kesi hiyo na baada ya wiki kutangaza kuwa vijana waliovamia duka lile walikuwa wamekamatwa.
Kwa mujibu wao kikosi cha maafisa wa uchunguzi wa Makosa ya jinai (DCI) kaunti ndogo ya Kilifi Kusini na maafisa wa Kituo cha polisi cha Mtwapa waliwakamata vijana watatu katika eneo la Vipingo, wakiwa katika nyumba ya Kiswahili wakiwa na bidhaa zilizizowahusishwa na kisa hicho.
Bw Mustafa Majeza Juma almaarufu mwenye umri wa miaka 21, Bubbline Kitsao Kazungu anayejulikana kama Kuta Girima wa miaka 26 na Abdul Mwatondo wa miaka 20, walikamatwa wakiwa na mapanga, bangi, mavazi ya kuficha uso wanapotekeleza wizi, simu na vitambulisho pamoja na risiti ya dhamana ya kesi ya wizi ya hapo awali.
Mahojiano ya washukiwa hao yalisababisha kukamatwa kwa washukiwa wengine watatu.
“Kupitia kwa jamii na uangalizi wa kanda za video za siri, tuliweza kuwafuatilia washukiwa na kuwapata katika maficho yao. Operesheni hiyo ilikuwa ya haraka na washukiwa wamezuiliwa katika kituo cha polisi cha Mtwapa wakisubiri kufikishwa mahakamani,” ikasema ripoti ya polisi.
Hata hivyo Inspekta Jenerali wa Polisi Douglas Kanja, amesema kuwa polisi wataendelea kukabiliana na uhalifu wa aina yote, akishukukuru umma kwa kutoa taarifa muhimu zinazoendelea kuimarisha sualama eneo hilo na kote nchini.
“Idara ya polisi itaendelea kulinda mali na wananchi na itaendelea kupamabana na uhalifu na inaomba wananchi kuendelea kuisaidia kufanya hivyo,” akasema msemaji wa Idara ya Polisi Muchiri Nyaga.