Habari za Kitaifa

Wajane wa Chepkut wapambana kwenye mzozo mkali wa mali ya Sh400 milioni

Na TITUS OMINDE February 10th, 2026 Kusoma ni dakika: 2

MZOZO wa urithi wa mali ya zaidi ya Sh400 milioni ya marehemu Mbunge wa zamani wa Ainabkoi William Chepkut umefika kortini huku wajane wake wawili wakimshutumu mke wa kwanza kwa kuwafungia nje na kuwanyima urithi.

Miaka minne baada ya kifo cha Bw Chepkut, wake wawili waliosalia wamemshutumu mke wa kwanza kwa kuwaweka gizani kuhusu mali iliyoko na kujaribu kuiuza hata kabla ya mchakato wa urithi kukamilika.

Juhudi za upatanishi zimekwama na sasa wake hao Dassie Ambassie na Betsy Birgen wameelekea kortini wakimshutumu mke wa kwanza Milcah Jepngetich kwa kujitwalia na kusimamia mali yote ya marehemu.

Bw Chepkut alishindwa kutetea ubunge wa Ainabkoi mnamo Agosti 2022 akiwa mwaniaji huru.

Aliaga dunia mnamo Oktoba 8, 2022 baada ya kuanguka nyumbani kwake jijini Nairobi.

Stakabadhi zilizoko mahakamani zilionyesha mwanasiasa huyo alikuwa na wake watatu, Milcah, Dassie na Betsy pamoja na watoto sita.

Mali inayozozaniwa ni shamba la kilimo Kaunti ya Uasin Gishu, hoteli mbili viungani mwa jiji la Eldoret, nyumba zinazopatikana mitaa ya Riverside na Westlands pamoja na ploti za mamilioni ya pesa Eldoret.

Juhudi za upatanishi hazikufanikiwa ndiposa kesi hiyo sasa imetua Mahakama Kuu ya Eldoret.

Kupitia Wakili Ndegwa Kiroku, Dassie na Betsy, walimwambia Jaji wa Mahakamu Kuu Reuben Nyakundi kuwa Milcah alikuwa akipanga kuuza sehemu ya mali hiyo licha ya kuwa kesi bado ipo mahakamani.

“Tumembiwa kuwa mshtakiwa ameweka tangazo la kuuza Hoteli ya Marriott kwenye barabara ya Eldoret-Kapsabet ambayo ina thamani ya Sh85 milioni. Tunaomba amri itolewe ya kuzima mauzo ya mali hiyo,” akasema Bw Kiroku mahakamani.

Kwa upande mwingine Milcah anasema kuwa walimiliki mali ambayo imezua mzozo pamoja na marehemu mumewe na wake wenza hawana haki ya kuidai.

Bw Kiroku aliongeza kuwa mteja wake anakabiliwa na hali ngumu kiuchumi kiasi kuwa amelemewa kuwalipia wanawe wawili karo akitaka apewe sehemu ya mali.

Milcah hata hivyo kupitia wakili wake amepuuza madai hayo. Kupitia wakili wake Diana Ndirangu, alimwambia Jaji Nyakundi kuwa hawatambui Dassie na Betsy kama wanaostahili kunufaikia mali ya marehemu.

Milcah anasema alikuwa kwenye ndoa na marehemu mbunge huyo kwa miaka 28 baada ya kufunga harusi Eldoret na wakajaliwa watoto wawili.

Bi Ndirangu pia alitaja madai kuwa Bi Milcah anapanga kuuza Hoteli ya Mariott kama ya uongo.

“Mali hiyo ilipatikana kwa juhudi zangu na mume wangu na haiwezi kudaiwa na yeyote,” akasema Milcah.

Jaji Nyakundi amesema kesi hiyo itasikizwa mnamo Februari 10, 2026.