Mhasibu mwenye ulemavu anavyotamba kwenye ufugaji kuku
WENGI walipomshauri Francis Muiruri atumie kipande chake cha ardhi Juja, Kaunti ya Kiambu, kujenga vyumba vya kupangisha, waliona hilo kama chaguo salama na lenye uhakika.
Kukusanya kodi kila mwisho wa mwezi ni ndoto ya Wakenya wengi.
Lakini kwa Francis, mahesabu hayo hayakuingiani, na kulingana naye, alitaka mradi utakaoingiza hela kila siku, ila si kusubiri wapangaji walipe ikizingatiwa kuwa wapo wanaochelewa kulipa kodi.

Aliingilia ufugaji wa kuku, uamuzi uliobadili kabisa maisha yake.
Leo, Francis anajulikana sana kama Francis Wa Kuku, mwanzilishi wa Francis Wa Kuku Digital Farm, ufugaji-biashara ambao umestawi kutoka kuku wachache hadi kuwa mradi mkubwa wa kibiashara unaosambaza mayai, kuku, vifaa vya kisasa kufuga kuku na mafunzo kwa wafugaji kote nchini.
Safari yake, hata hivyo, haijakuwa rahisi. “Nilizaliwa Kigio, Gatanga, Kaunti ya Murang’a, na nina ulemavu wa miguu unaonilazimu kutumia magongo kutembea,” anafunguka.

Kutia chumvi au msumari moto kwenye kidonda kinachouguza, kukata kiu cha elimu ilikuwa kibarua, na mara kadhaa alilazimika kuacha shule kutokana na umaskini uliogubika familia yake.
“Nilijifunza mapema kuwa maisha ya mtu mwenye ulemavu ni ghali na magumu zaidi,” anasema. Francis alisomea Joytown Special School, Thika, kabla ya kuacha shule kwa kukosa karo.
Kama watoto wengi waliokatiza masomo mapema, alihangaika kwa kazi za mikono na za sulubu, uchuuzaji wa bidhaa rejareja na kufuga kuku wachache alipomudu.
Hatimaye alirejea shuleni, akamaliza elimu ya msingi na sekondari, na baadaye kupata nafasi ya kusomea uhasibu (CPA).

Mwaka 2015 alipata ajira kama mhasibu katika Gatuzi la Kaunti ya Kiambu. “Ingawa nilikuwa na mshahara, niliamua kuendelea kufikiria kama mjasiriamali,” anaelezea.
Baada ya kuchukua mkopo kujenga nyumba kwao Gatanga msiba ulimkumba, mama yake alipopatikana na Saratani hali iliyomlazimu kuchukua mkopo mwingine wa Sh2.5 milioni kwa matibabu.
Wakati wa janga la Covid-19 mwaka 2020, upatikanaji wa mayai ulikuwa kibarua. Uwepo wa virusi vya corona nchini, licha ya athari zake ulifungua wamu nyingine ya maisha kwa Francis.
Anadokeza kwamba alinunua kuku wapatao 50. “Kijumla, ilinigharimu mtaji wa Sh50, 000 kuwanunua, kujenga mabanda na kununua chakula,” anaambia Akilimali Dijitali.

Anasema walikuwa wakitaga mayai 40 kwa siku, na soko lilikuwa tayari. Baada ya kifo cha mama yake, video fupi ya Francis akifuga kuku ilisambaa sana mitandaoni, ikimfungulia milango ya umaarufu na wateja.
“Mwanangu wa kiume ndiye alipakia video hiyo,” akafichua wakati wa mahojiano kwenye mradi wake Juja, eneo la Nyacaba.
“Kwa sababu haikuwa imeafikia ubora haswa kwa kutoa maelezo zaidi, nilitundika nyingine mitandaoni yenye maelezo kwa kina,” anaongeza.
Ni kupitia majukwaa ya intaneti, mhubiri maarufu Benson Gathungu (Mzee Kiengei), biashara yake ilipata msukumo mkubwa.

Anaelezea kwamba Pasta Kiengei, ambaye pia ni msanii wa vichekesho na mtangazaji, alimhoji kwenye redio – na huo ukawa mwanzo wa ufanisi wake. Alipata umaarufu, ufugaji wake ukajulikana na oda zikawa taratibu ya kila siku.
Leo hii, mradi wake una zaidi ya kuku 5,000 na nguruwe 200. “Karibu kuku 3,000 wanataga mayai kwa sasa, wakizalisha wastani wa trei 90 za mayai kwa siku,” Francis anafichua.
Kando na biashara ya mayai, Francis pia huuza kuku waliokomaa, chakula bora, mabanda ya kisasa (battery cages), na vifaranga wa miezi miwili waliopata chanjo kwa Sh1,000 kila mmoja.

Francis Wa Kuku Digital Farm imeajiri zaidi ya vijana 36 kwa njia ya moja kwa moja.
Amefanikiwa vipi kufikia alipo? Francis anajibu, “Ufugaji wa kuku ni biashara inayohitaji mkulima kuwa makini, mvumilivu, kuzingatia vigezo faafu kitaalamu na kuwa tayari kuwekeza kwa mifumo bora; kuanzia vizimba, chakula na matibabu.”
Aghalabu, Francis anathibitisha kwa nini ufugaji wa kuku una faida zaidi kuliko kujenga nyumba za kupangisha kama uwekezaji. Anasema, kwa kuku 100 pekee wanaofugwa katika nafasi ya futi 10 kwa 10, mfugaji anaweza kupata karibu Sh15, 000 kwa mwezi.
“Jaribu kujenga vyumba vya kupanga katika eneo hilo hilo uone ikiwa utapata faida kama hiyo,” anasema. Kwa ufugaji wa kuku, mapato hupatikana karibu kila siku.
