Sifuna njia panda maamuzi magumu yakimsubiri kuhusu mustakabali wake
KATIBU Mkuu wa ODM anayekabiliwa na utata Edwin Sifuna yuko njia panda kuhusu mwelekeo wa kisiasa atakaouchukua kabla ya 2027 huku akitathmini ule ambao unaweza kumjenga au kubomoa taaluma yake ya kisiasa.
Bw Sifuna anakabiliwa na hiari ya kusalia ODM, kuondoka chama hicho kisha kupambana kivyake kisiasa, kujiunga na mrengo wa Rais Mstaafu Uhuru Kenyatta hasa Jubilee. Pia ana hiari ya kujiunga na mrengo wa Kiongozi wa DCP Rigathi Gachagua.
Naibu huyo wa Kiranja wa Wengi kwenye Seneti wiki jana alifurushwa kama katibu mkuu wa ODM lakini akaelekea kortini na kupata afueni ya muda.
Alidai mahakamani kuwa hakupewa nafasi ya kutosha ya kujitetea kabla ya kufurushwa. Aidha, Jopo la Kutatua Mizozo kwenye Vyama vya Kisiasa nalo limpa nafuu zaidi baada ya kuzuia ODM kumwondoa madarakani. Jopo hilo lilikataa kutekeleza maafikiano ya ODM ya kumbandua Bw Sifuna ambayo yalitolewa mnamo Februari 11, 2026 jijini Mombasa.
Mbunge Mwakilishi wa Busia Catherine Omanyo aliteuliwa kama kaimu katibu mkuu kuchukua pahala pa Bw Sifuna.
Kuelekea mahakamani kunaashirikia kuwa Bw Sifuna yupo tayari kutumia ushawishi wa ODM kupambana ndani ya chama badala ya kukihama.
“Niko ODM na hakuna anayeweza kuniondoa wala sina nia ya kutoka. Si lazima ushikilie cheo ili kuwa mwanachama wa chama cha kisiasa,” akasema Bw Sifuna.
Hata hivyo, kusalia ODM kutakuja na changamoto zake kwa sababu lazima kunategemea iwapo chama kitaachana na mpango wa kushirikiana na Rais Ruto na kuenda kivyake 2027.
Kuendelea kukosa serikali kunaonekana kuwateka wafuasi wa ODM, baadhi wanaohisi kuwa Serikali Jumuishi haijawasaidia kivyovyote vile licha ya kuiunga mkono wakati Raila Odinga bado alikuwa hai.
Bw Sifuna anaonekana kushaajishwa na uungwaji mkono wa Gen Z na umati ambao umekuwa ukihudhuria mikutano yake na kumpa moyo aendelee na vita dhidi ya serikali.
Itakumbukwa kuwa mnamo Agosti 2025 pamoja na Mbunge wa Saboti Caleb Amisi, walitishia kuondoka ODM iwapo chama hicho kitaunga mkono Rais mnamo 2027.
“Niko tayari kutolewa kama katibu wa ODM kwa sababu nimesikia mtu mwengine anatayarishwa kuchukua wadhifa wangu. Siku ambayo watasema ODM imeamua kumuunga mkono mwaniaji wa UDA katika uchaguzi wa 2027, sitasoma maelewano au azimio hilo,” akasema Bw Sifuna wakati huo.
Umati ambao ulikwepo kwenye mkutano wa Bw Sifuna Busia na Kitengela umemkweza kisiasa huku vijana kwenye kikao cha Gen Z na Millenials wakiendelea kumshabikia.
Kwa mujibu wa Shirika la Takwimu Nchini (KNBS) kwenye sensa ya 2019, idadi ya vijana nchini hujumuisha zaidi ya asilimia 75 ya watu milioni 47.6 nchini.
Takwimu kutoka Tume Huru ya Uchaguzi na Mipaka Nchini (IEBC) zinaonyesha kuwa kulikuwa na wapiga kura 22,120,458 kufikia 2022.
Bw Sifuna amekuwa akionekana kuegemea Azimio na Jubilee huku pia akishirikiana na baadhi ya wanasiasa wa upinzani.
Pia amekuwa akimtetea Bw Kenyatta kutokana na madai kuwa rais huyo alishindwa kumpa marehemu Raila Odinga mamlaka mnamo 2022.
Uwepo wa Pauline Njoroge, ambaye ni naibu katibu mtendaji wa Jubilee Kitengelea kumeibua madai kwamba Bw Sifuna anapanga kushirikiana na Jubilee.
Hiari ya nne ya Bw Sifuna ni kuungana na Bw Gachagua ikizingatiwa DCP huenda ikapata uungwaji mkono wa Jamii ya Mlima Kenya katika Kaunti ya Nairobi.
Bw Sifuna analenga kutetea kiti chake cha useneta na tayari Mbunge wa Langáta Felix Odiwuor maarufu kama Jalangó, ametangaza kuwa atasaka nafasi hiyo mnamo 2027 kupitia ODM.
“Tunasubiri watu wengi wajiunge nasi akiwemo Seneta wa Nairobi Edwin Sifuna ambaye anataka kujiunga nasi,” akasema Bw Gachagua katika mazishi ya Mamake Mbunge wa Embakasi Kaskazini James Gakuya mwezi uliopita.
Bw Sifuna akiongea katika mazishi hayo alisema hatakubali mtu yeyote amchagulie marafiki, kauli iliyofasiriwa kama kushabikia upinzani.