Habari za Kitaifa

Wahuni wamelipwa kusababisha umwagikaji damu maadhimisho ya Juni 25, Gachagua adai

Na GITONGA MARETE, MERCY MWENDE June 24th, 2026 Kusoma ni dakika: 2

ALIYEKUWA Naibu Rais, Rigathi Gachagua, amedai kuwa Serikali inapanga kutumia nguvu na vitisho dhidi ya waandamanaji wanaotarajiwa kuingia barabarani kesho, na akawasihi vijana wa Gen Z kujiepusha na maandamano hayo.

Kiongozi huyo wa Chama cha Democracy for the Citizens Party (DCP) alisema ana taarifa anazodai ni za kuaminika kwamba, baadhi ya viongozi wa kisiasa wameajiri wahuni watakaojipenyeza miongoni mwa waandamanaji wa amani ili kusababisha vurugu na machafuko.

Akizungumza katika makazi yake ya Wamunyoro, Kaunti ya Nyeri, Jumanne, Gachagua alidai kuwa maafisa wa serikali wametenga mamilioni ya shilingi kufadhili magenge ya wahuni watakaotumika kuvuruga maandamano katika Jiji la Nairobi na eneo la Mlima Kenya.

Alitaja maafisa wakuu serikalini akiwemo Waziri wa Usalama wa Ndani Kipchumba Murkomen, Katibu wa Wizara ya Usalama wa Ndani Raymond Omollo, pamoja na viongozi wengine wanaomunga mkono Rais William Ruto, akiwalaumu kwa kupanga njama za kusababisha ghasia wakati wa maandamano hayo na baadaye kulaumu upinzani.

Alisema lengo la ghasia katika maeneo ya upinzani, hasa Mlima Kenya, ni kutoa taswira kwamba wakazi wa eneo hilo ndio pekee wanaopinga utawala wa Rais Ruto.

“Tuna taarifa kuwa Sh200 milioni zilitolewa asubuhi hii kutoka benki iliyoko Upper Hill kulipa wahuni ili kusababisha hofu katika Mlima Kenya na Nairobi. Polisi wameagizwa kuwasindikiza wahuni hao usiku, na magari ya abiria (matatu) yamekodishwa kusafirisha magenge ya wahalifu wanaojulikana,” alisema Gachagua.

Alidai kuwa baadhi ya maafisa wakuu wa polisi wamemuarifu kwamba wamepokea maagizo ya kutoingilia kati magenge hayo yakiharibu mali kabla ya baadaye kuwakamata wananchi na kuwafungulia mashtaka chini ya sheria za ugaidi.

“Maafisa hawa wametuambia kwa siri kwamba hawaridhiki na maagizo waliyopewa na Kipchumba Murkomen kwamba waondoke na waache wahuni waharibu biashara na kuwasha moto,” aliongeza.

Hata hivyo, aliyekuwa Naibu Rais huyo hakutoa ushahidi kuunga mkono madai hayo.

Mnamo Jumapili, Naibu Rais Kithure Kindiki alionya kuwa serikali haitakubali maandamano yatumiwe kupora mali na kuharibu miundombinu, akisema hatua kali zitachukuliwa dhidi ya watakaovunja sheria.

Alisisitiza kuwa hakuna nafasi kwa wahalifu kutumia maandamano kama kisingizio cha kufanya uhalifu, akiongeza kuwa Katiba inalinda kila raia, wakiwemo wasioshiriki maandamano.

“Siku ya Alhamisi hakutakuwa na nafasi ya mchezo wowote usiofaa katika Jamhuri ya Kenya. Hakuna mtu atakayetulaumu kwa kushindwa kulinda Wakenya wanaofanya biashara, wanaosafiri au wanaoendelea na shughuli zao mbali na maandamano,” alisema Kindiki.

Alizungumza alipohudhuria ibada ya kidini na kuchangisha fedha kwa makanisa 19 katika eneo la Kapsang, Soy, Kaunti ya Uasin Gishu.

“Maandamano yanaruhusiwa na Katiba. Lakini hakutakuwa na nafasi kwa yeyote kuvunja haki za wengine, kupora au kushambulia Wakenya wengine. Kila mtu atalindwa, wale wanaoshiriki maandamano na wale wasioshiriki,” aliongeza.

Waziri wa Usalama wa Ndani Kipchumba Murkomen naye Jumatatu alionya kuwa hawataruhusu watakaojaribu kusababisha vurugu, lakini akasisitiza kuwa maandamano ya amani yataruhusiwa chini ya ulinzi wa polisi.

Akizungumza katika makazi yake ya Wamunyoro alipokutana na ujumbe wa viongozi kutoka Kaunti ya Kiambu, Gachagua alisema ana hofu kuhusu maisha ya vijana wa Kenya, na akawaomba wasiende barabarani.

Kauli yake inafuatia maandalizi ya maandamano ya vijana wa Gen Z ambao wameendelea kupanga mikutano ya kupinga masuala ya utawala, uwajibikaji na hali ya uchumi.

Kiongozi huyo wa DCP aliwaomba vijana wa Kenya kufikiria upya mipango yao ya maandamano akisema usalama wao unapaswa kupewa kipaumbele.

“Kuna njia ya kikatiba ya kuondoa serikali kupitia sanduku la kura mwaka ujao,” alisema.

Aliwahimiza Wakenya wasioridhika na serikali ya sasa kutoa maoni yao katika uchaguzi mkuu wa 2027 badala ya kuhatarisha maisha yao barabarani.

Gachagua pia aliwataka wafanyabiashara wa Nairobi na eneo la Mlima Kenya kuwa makini, akidai kuwa watu kutoka nje ya maeneo hayo wamepangwa kuharibu mali wakati wa maandamano.

“Msiruhusu watu kutoka nje ya jamii zenu kuharibu biashara na nyumba zenu,” alisema.