Habari

Ida sasa aambia bunge ako tayari kukalia kiti cha UNEP

Na SAMWEL OWINO February 21st, 2026 Kusoma ni dakika: 1

MASWALI kuhusu uwezo wake wa kitaaluma, maarifa na tajriba katika kushughulikia changamoto za mabadiliko ya tabianchi yalitawala kikao cha Bunge cha kumpiga msasa Bi Ida Odinga kama balozi wa Kenya katika Shirika la Umoja wa Mataifa kuhusu Mazingira (UNEP).
Akiwa mbele ya Kamati ya Bunge kuhusu Ulinzi, Ujasusi na Mahusiano ya Kigeni, Bi Odinga aliulizwa hatua mahsusi atakazochukua kuiweka Kenya katika ramani ya kimataifa ya mazingira iwapo ataidhinishwa.
Wabunge walitaka kujua atakavyobadili mwelekeo kutoka taaluma ya elimu na mashirika ya kiraia hadi diplomasia, inayohitaji ustadi wa majadiliano na ushawishi wa kimataifa.
Bi Odinga aliambia kamati inayoongozwa na Mbunge Nelson Koech kuwa, tajriba yake kama mwalimu wa jiografia na kushiriki shughuli za uhifadhi wa mazingira imemjengea msingi thabiti. Alitaja ushirikiano wake na marehemu mshindi wa Tuzo ya Amani ya Nobel Wangari Maathai katika kampeni ya kupanda miti.
Mbunge wa Kamukunji Yusuf Hassan aliibua suala la uhaba wa rasilmali katika Umoja wa Mataifa kufuatia baadhi ya mataifa kupunguza ufadhili, akimtaka aeleze atakavyoongeza rasilmali za UNEP.
Bi Odinga alisema atategemea mtandao wa wataalamu na uzoefu wake katika kusaka pesa ndani na nje ya nchi.