Kimataifa

Serikali ya Rais Gen Z Nepal yaanza kuwaandama waliopora nchi

Na REUTERS June 23rd, 2026 Kusoma ni dakika: 1

KATHMANDU, Nepal:

ALIYEKUWA Waziri wa Fedha wa Nepal Bishnu Prasad Paudel alinyakwa mnamo Jumatatu kuhusiana na mashtaka ya ulanguzi wa fedha.

Hatua hiyo inakuja wakati utawala wa Gen Z ambao ulichukua usukani nchini humo Machi, unaendelea kuwaandama viongozi walioshiriki ufisadi na kujilimbikizia mali katika utawala uliopita.

Paudel, 66, ambaye ni kiongozi wa ngazi ya juu wa Chama cha Nepal (UML) na kigogo katika uliokuwa utawala uliopita wa K.P Sharma Oli, alizuiliwa kwenye hoteli moja, Magharibi mwa Nepal.

Msemaji wa Polisi Abi Narayan Kafle alisema Paudel alikuwa akipelekwa Kathmandu ili akabidhiwe kwa Idara ya Ulanguzi wa Fedha.

Kukamatwa kwake kunatokea baada ya serikali ya Oli kuondolewa madarakani kutokana na wimbi la maandamano ambalo lilitingisha nchi hiyo.

Katika maandamano hayo zaidi ya watu 76 waliuawa na zaidi ya wengine 2,500 wakajeruhiwa. Pia majengo mengi ya serikali yakiwemo bunge, yaliteketezwa.

Oli na waziri wake wa masuala ya nyumbani, walikamatwa kwa kushindwa kuzuia ghasia hizo. Wawili hao kwa sasa wapo nje kwa dhamana.

Waziri Mkuu Balendra Shah, 36, ambaye ni mwanamuziki wa kufokafoka na mwanasiasa, alichukua usukani mnamo Machi na akaahidi kupambana na ufisadi. Pia aliahidi kuwaandama viongozi ambao walihusika na uvunjaji wa haki katika utawala uliopita.