Wamiliki wa hoteli inayojengwa karibu na Ikulu ni Kihika na mumewe, Taifa Leo yabaini
HOTELI ya kifahari ya mabilioni ya fedha ya Encore iliyojengwa karibu na Ikulu ya Nakuru inamilikiwa na Gavana wa Nakuru Susan Kihika na mumewe Sam Mburu, Taifa Leo imebaini.
Siku moja baada ya wabunge kuibua wasiwasi kuhusu ongezeko la majengo marefu karibu na Ikulu ya Nakuru, ikiwemo hoteli hiyo ya kifahari iliyo na zaidi ya vyumba 200, Bw Mburu alithibitisha kuwa yeye ndiye mmiliki wa jengo hilo.
Katika mahojiano ya simu na Taifa Leo, Bw Mburu alisema alipata idhini zote muhimu kutoka kwa serikali ya kaunti na mashirika ya kitaifa kabla ya ujenzi kuanza.
“Ninathibitisha kuwa mimi ndiye mmiliki wa Encore Hotel na nilipata vibali vyote vinavyohitajika kabla ya ujenzi kuanza. Mradi wa kiwango hiki huhitaji vibali sahihi, na tulivipata vyote,” alisema bila kutoa maelezo zaidi.
Alisisitiza kuwa eneo la hoteli hiyo haliathiri usalama wa Ikulu ya Nakuru kwa kuwa ilipata kibali kinachohitajika.
Mwenyekiti wa Chama cha Utalii Nakuru Mchungaji David Mwangi, ambaye pia ni msimamizi wa mradi huo, alisema walipata vibali vyote muhimu, ikiwemo kibali cha tathmini ya athari za mazingira kutoka Mamlaka ya Kitaifa ya Kusimamia Mazingira (NEMA), pamoja na idhini ya mipango ya ujenzi kutoka serikalini.