Magavana wasisitiza watasusia kamati ya Seneti
BARAZA la Magavana (CoG) limetangaza kuwa magavana hawatahudhuria vikao vya Kamati ya Seneti ya Hesabu za Kaunti (CPAC) hadi madai ya hongo, vitisho na unyanyasaji yanayowahusisha baadhi ya wanachama wa kamati hiyo yashughulikiwe kikamilifu.
Katika barua aliyoandikia Spika wa Seneti, Amason Kingi, Mwenyekiti wa CoG Ahmed Abdullahi, alisema uamuzi huo ulifikiwa katika kikao maalum cha baraza hilo.
Alisema magavana wako tayari kufika mbele ya kamati zote za Seneti kujadili masuala yanayohusu kaunti, isipokuwa CPAC, hadi malalamishi waliyowasilisha hapo awali yatatuliwe.
Katika barua hiyo, magavana walieleza kuwa tayari waliwasilisha malalamishi rasmi kuhusu tabia ya baadhi ya maseneta wa CPAC, wakitaja madai ya ulaghai wa fedha, vitisho, kuwindwa kisiasa na dhuluma.
“Tabia hiyo inaonyesha dharau kwa mamlaka na heshima ya serikali za kaunti, na pia inadhoofisha hadhi ya Seneti kama taasisi ya kikatiba,” ilisema sehemu ya barua hiyo.
Hata hivyo, Spika Kingi aliahirisha kikao cha maridhiano kilichokuwa kimepangwa siku hiyo, akisema kuwa kufika kwa magavana mbele ya kamati hakuwezi kujadiliwa.
Alionya kuwa kususia vikao kunadhoofisha jukumu la usimamizi la Seneti chini ya Ibara ya 96 ya Katiba, na pia kunakiuka Ibara ya 125 inayoruhusu Bunge kuwaita mashahidi kufika mbele yake.
Mzozo huo umeathiri pia Kamati ya Uwekezaji wa Kaunti na Hazina Maalum (CPIC), huku kamati zote mbili zikiendelea kupitia ripoti za Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali, Bi Nancy Gathungu, za mwaka wa fedha 2024/25.
Kwa mujibu wa Ibara ya 229(4) ya Katiba, ripoti hizo zinapaswa kukamilishwa kufikia Machi 31.
Akizungumza akiwa Kilifi mwezi uliopita, Bw Abdullahi alisema magavana hawatafika mbele ya kamati inayoongozwa na Seneta wa Homa Bay, Moses Kajwang, hadi malalamishi yao yashughulikiwe kupitia mazungumzo.