Serikali yatoa tahadhari kwa raia wake wanaoishi Mashariki ya Kati
SERIKALI ya Kenya jana ilitoa ushauri wa kiusalama kwa raia wake wanaoishi au kusafiri Ukanda wa Mashariki ya Kati ikiwataka wachukue tahadhari kutokana na vita kati ya Iran, Israel na Amerika.
Tahadhari hiyo iliyotolewa na Wizara ya Masuala ya Kigeni inatokea wakati ambapo vita vimechacha huku Israel na Amerika zikishambulia Iran ambayo pia imekuwa ikilenga vituo vya kijeshi vya Amerika ukanda wa Mashariki ya Kati.
Mnamo Jumamosi usiku, shambulizi la Amerika lilimuua Kiongozi wa Kidini wa Iran Ayatollah Khamenei na nchi hiyo imetangaza kuwa inajiandaa kulipiza kisasi mauaji hayo.
Kuendelea kwa vita hivyo kumeibua hofu kuhusu raia wa Kigeni wanaoshi Mashariki ya Kati.
Serikali jana iliwataka Wakenya wanaoishi Iran, Israel, Qatar, Mmilki ya Kiarabu, Bahrain, Kuwait, Saudi Arabia, Jordan na Iraq wachukue tahadhari kuhusu usalama wao na wawasiliane nao wakihisi kuna hatari inayowakodolea macho.
Serikali iliwataka Wakenya hao wajizuie kutembea kiholela, kuwataka wasifike karibu na kambi za kijeshi au maeneo ambako umma umekusanyika ambayo yanaweza kulengwa kupitia mashambulizi.
Vilevile serikali ilitoa wito kwa Wakenya wazingatie mwongozo wa kiusalama ambao unatolewa katika nchi wanakoishi na kuwa ange kuhusu mawasiliano yoyote yanayotolewa.
Tayari vita hivyo vimesababisha nchi kadhaa kufunga nyuga zao za ndege ambapo safari kadhaa zimefutiliwa mbali.
Wakenya wametakiwa pia kuweka sikio nje kuhusu mpango wowote wa kuwahamisha kutoka maeneo ambayo ni hatari na yanaweza kuathiriwa na vita.
“Wakenya ambao bado hawajajisajili wafanye hivyo na ubalozi ambao upo karibu nao ili wawe wakipata taarifa kutoka kwa ubalozi huo kwa wakati,” ikaongeza ushauri huo.
Wizara hiyo pia ilitoa nambari za mawasiliano kwenye ubalozi wa Kenya Tehran, Tel Aviv pamoja na miji ya Kuwait, Muscat, Doha, Riyadh, Jeddah, Abu Dhabi na Dubai.
“Wizara ya Masuala ya Nje inaendelea kutathmini hali na kuwasiliana na ubalozi wake katika nchi hizi. Tutatoa taarifa zaidi kupitia mitandao yetu inayotambulika,” akasema Waziri wa Masuala ya Nje Musalia Mudavadi.