Kimataifa

Trump aonya Iran dhidi ya kulipiza kisasi baada ya Amerika-Israel kuangamiza Ayatollah

March 2nd, 2026 Kusoma ni dakika: 3

TEL AVIV/DUBAI, Israel

ISRAEL imesema imetekeleza msururu mwingine wa mashambulizi dhidi ya Iran huku raia wa Iran wakigubikwa na suitafahamu baada ya kiongozi wao mkuu wa kiroho, Ayatollah Ali Khamenei, kuuawa kwenye mashambulizi ya Amerika na Israel, huku Rais Donald Trump akionya iwapo ulipizaji kisasi utafanywa.

Saa kadhaa baada ya mataifa hayo mawili kusema shambulizi la angani lilimuua Khamenei katika operesheni ya jeshi ya kung’atua mamlakani serikali ya Jamhuri ya Kiislamu (IS), kituo cha habari Iran kilithibitisha kifo cha kiongozi huyo mwenye umri wa miaka 86, Jumamosi.

Katika pigo kuu jingine kwa viongozi wa Iran, Mkuu wa Wafanyakazi wa Jeshi, Abdolrahim Mousavi, aliuawa kwenye mashambulizi hayo, ilisema Iran TV.

Amerika itashambulia Iran “kwa pigo ambalo halijawahi kamwe kuonekana hapo mbeleni,” Trump alionya Jumapili, ikiwa taifa hilo la Mashariki ya Kati litalipiza kisasi.”

“Iran imesema itashambulia vikali leo, kwa nguvu zaidi kuliko ilivyowahi kushambuliwa awali,” alisema Trump kupitia ujumbe kwenye mtandao wa Truth Social.

Alisema, “Itakuwa bora zaidi wasifanye hivyo, kwa sababu wakifanya hivyo, tutawashambulia kwa nguvu ambazo hazijawahi kuonekana kamwe hapo awali!”

Afisa mkuu wa usalama Iran, Ali Larijani, alisema baraza la muda la uongozi litabuniwa.

Alishutumu Amerika na Israel kwa kujaribu kupora na kugawanya Iran akionya “makundi yanayounga mkono mapinduzi” kuhusu adhabu kali ikiwa yatajaribu kuchukua hatua, ilisema runinga ya kitaifa.

Kwenye matamshi yaliyomlenga Trump na mwandani wake, Waziri Mkuu wa Israel Benjamin Netanyahu, Spika wa Bunge la Iran, Mohammad Baqer Qalibaf, alisema amevuka mpaka hatari na “watalipia”.

Duru zinazofahamu kuhusu operesheni ya Israel zilieleza Reuters kwamba hakuna mabadiliko kwenye mikakati ya jeshi baada ya mauaji ya Khamenei na mashambulizi yataendelea kuwalenga maafisa wa Iran na miundomsingi ya makombora.

Milipuko mikubwa ilisikika kwa siku ya pili Jumapili katika kituo cha kibiashara cha kiukanda, Dubai na jiji kuu la Qatar, Doha, walisema mashahidi, baada ya Iran kutekeleza mashambulizi ya kulipiza kisasi katika mataifa jirani ya ghuba.

Mawimbi ya moshi mweupe kutokana na makombora yaliyozuiwa yalitanda hewani Dubai huku miale ya moshi mweusi ikipanda kwenye bandari yake ya Jebel Ali, moja kati ya vituo vyenye shughuli nyingi zaidi Mashariki ya Kati.

Iran iliyokuwa imesema italenga Amerika ikiwa ngome zake zitashambuliwa, ililenga vituo anuwai hasa kambi za kijeshi na kutikisa ghuba hiyo yenye utajiri wa mafuta.

Trump alisema mashambulizi ya angani yalilenga kumaliza tishio la miongo mingi la Iran na kuhakikisha haitaunda silaha za kinuklia.

“Hii si haki kwa watu wa Iran tu, lakini kwa Waamerika wote, na watu kutoka mataifa mengi duniani kote, ambao wameuawa au kujeruhiwa na Khamenei na genge lake la wauaji,” Trump aliandika kwenye Truth Social.

Trump na Netanyahu waliwaeleza wananchi wa Iran kutumia fursa hiyo nadra kuwang’oa mamlakani viongozi wao wa kidini.

Utawala wa miaka 36 wa Ayatollah Ali Khamenei uliunda Iran kuwa taifa lenye nguvu zaidi linalopinga Amerika, ukieneza ushawishi wake kote Mashariki ya Kati, huku ukitumia udikteta kuangamiza misukosuko iliyozuka mara kwa mara Iran.

Khamenei aliuawa Jumamosi akiwa na umri wa miaka 86, idhaa ya kitaifa Iran ilitangaza, katika mashambulizi ya angani yaliyotekelezwa na Israel na Amerika yaliyogeuza mavumbi kituo chake kikuu jijini Tehran, baada ya miongo mingi ya juhudi za kusuluhisha kidiplomasia mzozo kuhusu mpango wa nuklia kufeli.

Khamenei ambaye mwanzoni alipuuzwa kama mtu dhaifu asiyeweza kufanya maamuzi magumu, alionekana kama chaguo lisilowezekana la kiongozi wa kiroho kufuatia kifo cha kiongozi mkakamavu, Ayatollah Ruhollah Khomeini, aliyebuni Jamhuri ya Kiislamu ya Iran.

Lakini kuinuka kwake kwenye kilele cha mpangilio wa utawala nchini, kulimkabidhi mamlaka makubwa kuhusu masuala ya kitaifa.

Khamenei alikuwa “ajali ya historia” aliyekwenda kutoka “rais dhaifu kuwa kiongozi mkuu wa kiroho aliyeanza kama mtu dhaifu hadi moja kati ya raia watano wa Iran wenye nguvu zaidi katika miaka 100 iliyopita,” Karim Sadjadpour katika Taasisi ya Carnegie Endowment for International Peace alieleza Reuters.

Ayatollah Khamenei alikashifu Washington katika utawala wake wote, akiendeleza ukosoaji wake baada ya mwanzo wa hatamu ya pili ya Donald Trump kama rais wa Amerika, 2025.