Habari za Kitaifa

ODM yazozana vikali kuhusu makataa na UDA: ‘Kurefusha mkataba kwahitaji saini ya Baba’

Na MOSES NYAMORI, DANIEL OGETTA March 3rd, 2026 Kusoma ni dakika: 2

MALUMBANO yameibuka kati ya mirengo mbalimbali ndani ya ODM kuelekea makataa ya Machi 7 ya muafaka uliotiwa saini kati yao na UDA.

Kutiwa saini kwa muafaka huo mwaka jana kulishuhudiwa na Rais William Ruto pamoja na aliyekuwa Kiongozi wa ODM marehemu Raila Odinga.

Katika mkataba huo, viongozi hao waliorodhesha masuala 10 ambayo yangetekelezwa ndani ya mwaka moja.

Mrengo unaounga mkono Kiongozi wa ODM Dkt Oburu Oginga unasema hakuna shinikizo na Machi 7 itakuwa tu ya kuadhimisha mwaka mmoja wa muafaka.

“Wengine wanawapotosha wafuasi wetu kuwa mnamo Machi 7 tutatengana rasmi na serikali. Siku hiyo tutakuwa na ripoti kuhusu hatua zilizoafikiwa katika kutekeleza ajenda hizo 10,” akasema Dkt Oginga mjini Migori wikendi iliyopita.

Hata hivyo, Katibu Mkuu wa ODM Edwin Sifuna akizungumza na runinga mmoja nchini alisema muafaka huo haukuwa na muda wa kurefushwa na unastahili kutekelezwa ndani ya mwaka moja.

“Mtu yeyote ambaye anataka kurefusha mkataba lazima aende Bondo na apate saini ya Baba. Hakuna saini yeyote itawekwa kwenye muafaka huu kwa sababu Raila hakuomba urefushwe,” akasema Bw Sifuna.

Naye Seneta wa Vihiga Godfrey Osotsi ambaye ni mkosoaji mkubwa wa Rais William Ruto, alisema Kenya Kwanza ndiyo imekuwa ikitatiza utekelezaji wa ajenda 10 zilizoko kwenye muafaka huo.

Bw Osotsi alisema hakuna mwaathiriwa wa ukatili wa polisi ambaye amelipwa fidia na serikali bado inaendelea kuvuruga vyama dhabiti vya kisiasa kama ODM.

“Hakuna mwanya wa kurefusha mkataba huo na wa kulaumiwa ni Ruto na viongozi wa ODM ambao wanarindima ngoma ya ‘Tutam’. Madai yao kuwa watakuwa wanatoa ripoti hayako mahala popote kwenye muafaka,” akasema.

Mtaalamu kuhusu masuala ya uongozi Profesa Gitile Naituli asema ajenda 10 hazijatelelezwa na muafaka huo haukuwa na mashiko.

“Mkataba huo ulitumiwa tu na ODM kuingia serikalini baada ya kuwasaliti Gen Z katika maandamano ya 2024,” akasema Profesa Naituli.

Msomi huyo anasema ajenda hizo 10 ni masuala ambayo yalikuwa yakipiganiwa pia na Gen Z na ODM ilijikita pia katika mambo hayo kutokana na historia yake ya ukombozi.

Mwenyekiti wa Kamati ya Bajeti katika Bunge la Kitaifa Samuel Atandi naye anasema mengi yaliyomo kwenye muafaka huo yametekelezwa.

Alitoa mfano wa mgao kwa kaunti ambapo Sh415 bilioni zimetengewa magatuzi hayo na kiasi hicho kitapandishwa hadi Sh450 bilioni ndani ya mwaka mmoja.