NTSA yakosolewa kwa misururu ya makosa ya sera na utekelezaji
MAMLAKA ya Kitaifa ya Usafiri na Usalama Barabarani (NTSA) inakosolewa vikali na madereva, viongozi na wadau wa sekta ya usafiri kutokana na kile kinachoelezwa kuwa makosa ya mara kwa mara katika kutunga na kutekeleza sera zake.
Mjadala mkubwa sasa unahusu mpango wa kuanzisha ukaguzi wa lazima wa kila mwaka kwa magari ya kibinafsi yenye umri wa zaidi ya miaka minne.
Hata hivyo, NTSA imelazimika kusimamisha utekelezaji wa agizo hilo hadi mwanzoni mwa mwaka ujao baada ya kukumbana na upinzani mkali.
Mkurugenzi Mkuu wa NTSA Nashon Kondiwa amesema magari ya kibinafsi na pikipiki yanachangia asilimia 62 ya ajali nchini, hivyo ukaguzi huo unalenga kuboresha usalama barabarani na kuimarisha sajili ya kitaifa ya magari.
Lakini wadau wamekosoa mamlaka hiyo kwa kutangaza utekelezaji wa sheria mpya bila kuwa na miundombinu ya kutosha.
Bw Kondiwa alikiri kuwa kwa sasa kuna vituo 17 pekee vya serikali vya ukaguzi wa magari nchini, huku NTSA ikitarajia kuongeza idadi hiyo hadi zaidi ya 100 mwaka ujao.
Wakili Steve Kabita alisema NTSA ilifanya makosa kwa kuanzisha utekelezaji wa sheria bila kuwa tayari.
Chama cha Wamiliki wa Magari Kenya (MAK) pia kilisema mamlaka hiyo haina uwezo wala msingi wa kisheria wa kukagua mamilioni ya magari ya kibinafsi kila mwaka.
Mzozo huo umeongezeka baada ya kubainika kuwa NTSA ilianza kutekeleza kanuni hizo kabla ya Seneti kuzipitisha. Maseneta wameonya kuwa hatua hiyo ni kinyume cha Katiba na wametishia kuipeleka mahakamani.
Kiongozi wa Wachache Seneti Stewart Madzayo alisema kanuni hizo hazina nguvu za kisheria kwa kuwa bado hazijapitishwa na Seneti.
Naye Seneta wa Makueni Dan Maanzo alisema Seneti itazitupilia mbali ili kuwalinda Wakenya dhidi ya gharama zisizo za lazima.
Mbali na suala la ukaguzi wa magari, NTSA imekuwa ikikosolewa kwa matatizo mengine.
Ripoti ya Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali Nancy Gathungu ilionyesha dosari katika mfumo wa kidijitali wa TIMS unaosimamia usajili na uhamishaji wa umiliki wa magari, hali inayoweza kusababisha kupotea kwa mapato.
Aidha, mamlaka hiyo imekuwa ikilaumiwa kwa kuchelewesha utoaji wa nambari za usajili wa magari na utekelezaji wa miradi iliyokwama mahakamani, ikiwemo leseni mpya za kidijitali na mfumo wa faini za moja kwa moja kwa wanaokiuka sheria za trafiki.
Ingawa NTSA inasema hatua hizo zinalenga kuimarisha usalama barabarani, viongozi na wadau wanasisitiza kuwa sera hizo zinapaswa kuandaliwa kwa kushirikisha wananchi kikamilifu na kuzingatia uwezo wa utekelezaji kabla ya kuanza kutumika.