Matumaini ya huduma bora polisi wakiongezwa donge nono kwenye mishahara
MAAFISA wa polisi wa ngazi za chini ndio watanufaika pakubwa na nyongeza ya mishahara chini ya mageuzi yanayoendelea katika sekta ya usalama, ambapo makonstebo watapokea ongezeko kubwa zaidi.
Marekebisho haya ni sehemu ya mapendekezo ya jopo la mageuzi ya polisi lililoongozwa na aliyekuwa Jaji Mkuu, David Maraga, ambalo liliwasilisha ripoti yake kwa Rais William Ruto mwishoni mwa 2023.
Awamu ya mwisho ya nyongeza hii itaanza kutekelezwa Julai mwaka huu, ikihitimisha mpango wa miaka mitatu wa kutathmini upya mishahara ya maafisa wa Huduma ya Kitaifa ya Polisi Kenya, Huduma ya Magereza Kenya, na Huduma ya Vijana kwa Taifa (NYS).
Mageuzi haya yanasimamiwa na Katibu wa Wizara ya Usalama wa Ndani, Raymond Omollo, ambaye pia ni mwenyekiti wa Kamati ya Kitaifa ya Utekelezaji wa Mageuzi katika sekta ya usalama.
Katika taarifa iliyotoa jana, kamati ilithibitisha kuwa awamu ya mwisho ya nyongeza ya mishahara itaanza Julai.
Nyongeza hii ni sehemu ya mfumo wa mageuzi wenye nguzo nne unaolenga kuimarisha uwezo wa taasisi, utendaji, uwajibikaji na usimamizi maafisa.
Kati ya hatua hizi, ustawi wa maafisa, ukiwemo mshahara, bima ya afya na makazi. umepewa kipaumbele kikubwa.
Takwimu zinaonyesha kuwa maafisa wa ngazi za chini na kati, watanufaika pakubwa. Kwa mfano, konstebo wa polisi, ambaye ni afisa wa ngazi ya chini zaidi, atapokea mshahara wa juu wa Sh57,700 kutoka Sh38,975, sawa na ongezeko la asilimia 48.
Maafisa wapya wanaoanza kazi watapokea mshahara wa kuanzia Sh29,296 kutoka Sh20,390, ongezeko la asilimia 44.
Walio katika kundi la mishahara la PG9 ni miongoni mwa watakaonufaika pakubwa, ambapo mshahara wa chini unaongezwa kutoka Sh68,720 hadi Sh111,906 na mshahara wa juu kupanda hadi Sh148,538, ongezeko la zaidi ya Sh50,000.
Walio katika makundi ya kati kama PG8, PG7, PG6 na PG5 pia wamenufaika kwa ongezeko kubwa, hatua inayopunguza pengo kati ya viwango vya chini na vya kati.
Kwa upande mwingine, maafisa wa ngazi ya juu watapata ongezeko la wastani. Afisa wa juu zaidi katika polisi atapokea Sh345,850 kwa mwezi kutoka Sh289,090, ongezeko la asilimia 20.
Aidha, Rais Ruto alithibitisha kuwa maafisa wa Huduma ya Magereza Kenya pia watanufaika, huku maafisa wa juu zaidi wa magereza wakipata kati ya Sh301,548 hadi Sh584,903 kutoka kiwango kilichokuwa kati ya Sh292,765 hadi Sh576,120.
Wale wa vyeo vya chini watapokea ongezeko linalofanana na la maafisa wa polisi.
Katibu Omollo alisema polisi na maafisa wote wanastahili kufanya kazi katika mazingira mazuri.
Serikali pia inaendelea kutoa vifaa, magari, teknolojia, nyumba, na bima ya afya na maisha kwa maafisa wake.
Pia, zaidi ya nyumba 47,000 zinajengwa chini ya Mpango wa Makazi Nafuu ili kushughulikia uhaba wa makazi kwa maafisa wa usalama.
Akizungumza na Taifa Leo kuhusu nyongeza ya mishahara, Dkt Omollo alisema kuwa maafisa wa polisi, wanastahili kufanya kazi katika mazingira mazuri na ustawi wao lazima uzingatiwe ipasavyo.
“Maafisa wa polisi pia wanapaswa kusaidiwa kwa vifaa, magari na pia kwa teknolojia,” alisema Dkt Omollo.
Aliongeza kuwa, “Utawala wa Rais Ruto, kama unaendelea kikamilifu kuhakikisha mageuzi haya ya usalama yanatekelezwa kama walivyoahidiwa.”
Katibu huyo alisema kuwa serikali ipo katika mwelekeo sahihi wa kutekeleza mageuzi kadhaa katika sekta ya usalama na “nyongeza ya mishahara ni mojawapo ya matokeo halisi ya jitihada za kuboresha sekta hiyo.”