Viongozi waungana Pwani kuvumisha Tutam
MAWAZIRI wa Michezo na Vijana, Bw Salim Mvurya, mwenzake wa Madini, Bw Hassan Joho, pamoja na Spika wa Seneti, Bw Amason Kingi, wamewahimiza wakazi wa pwani kumuunga mkono Rais William Ruto i katika Uchaguzi Mkuu wa 2027.
Viongozi hao walisema Rais Ruto amejitolea kuinua eneo la Pwani kimaendeleo bila kujali kuwa hakupata kura nyingi kutoka eneo hilo katika uchaguzi mkuu wa 2022.
Wakizungumza katika mkutano wa kisiasa uliofanyika Malindi, viongozi hao walisema Rais Ruto anatarajiwa kutoa zaidi ya hati miliki 200,000 kwa wakazi wa pwani ili kumaliza changamoto ya umiliki wa ardhi ambayo imekuwa ikiwakumba kwa miaka mingi.
Waziri Salim Mvurya alisema serikali ya Rais Ruto imeanzisha na kuendeleza miradi mbali mbali ya maendeleo, ikiwemo uchumi wa baharini, ujenzi wa barabara, pamoja na kufufua shughuli za Bandari ya Mombasa, ambayo waliitaja kuwa uti wa mgongo wa uchumi wa ukanda wa Pwani.
“Ijapokuwa Rais Ruto hakupata kura nyingi kutoka Pwani mwaka wa 2022, eneo hili limefaidika pakubwa na serikali yake. Amehakikisha wapwani wanashirikishwa katika maendeleo na katika meza za maamuzi ya kitaifa. Hadi sasa ameteua zaidi ya wapwani 106 kuhudumu katika serikali kuu,” alisema Bw Mvurya.
Aliongeza kuwa serikali imetenga Sh5 bilioni kwa ajili ya kushughulikia tatizo la ardhi katika eneo la Pwani kupitia ununuzi wa mashamba kutoka kwa wamiliki wakubwa na kuyagawa kwa wananchi wasiokuwa na ardhi.
“Ndio maana sisi kama viongozi wa Pwani tumeamua kuchukua msimamo wa pamoja. Tunaamini ushirikiano huu utaendelea kuwaletea wananchi maendeleo zaidi,” alisema Waziri Mvurya.
Bw Mvurya alisema yeye, Bw Joho na Spika Kingi wameamua kuweka kando tofauti zao za kisiasa na kuungana katika kampeni za kuhamasisha wananchi kuunga mkono serikali ya Kenya Kwanza.
“Zamani ilikuwa vigumu kuona viongozi kutoka vyama tofauti kama ODM, UDA na PAA wakifanya kampeni pamoja. Lakini baada ya Rais Ruto na Raila Odinga kuamua kushirikiana kwa maslahi ya taifa, nasi tumeamua kufanya kazi pamoja kwa manufaa ya wananchi,” alisema.
Aliwataka wakazi wa Pwani kutowaunga mkono viongozi wa upinzani, akidai kuwa hawakutatua changamoto za eneo hilo walipokuwa serikalini.
Kwa upande wake, Waziri wa Uchumi wa Samawati, Bw Hassan Joho, alisema kwa miaka mingi wapwani wamekuwa wakipuuzwa kisiasa, lakini hali hiyo sasa imebadilika.
“Hatuchezi tena siasa za zamani. Mambo yamebadilika. Msifanye maamuzi kwa hisia. Wapo viongozi waliokuwa serikalini kwa zaidi ya miaka 20 lakini hawakutatua matatizo ya Pwani,” alisema.
Bw Joho alisema serikali imejizatiti kutatua tatizo la ukosefu wa ardhi na kuwasihi wakazi wa Pwani kuendelea kuiunga mkono badala ya kusikiliza viongozi wa upinzani.
Naye Spika wa Seneti, Bw Amason Kingi, aliwataka wakazi wa Pwani kumpa Rais Ruto kura nyingi katika uchaguzi ujao, akisema ndiyo njia ya kuthamini maendeleo ambayo serikali yake imepeleka eneo hilo.
Alisema kati ya marais wote waliowahi kuongoza Kenya, hakuna ambaye amewekeza katika maendeleo ya Pwani kwa kiwango sawa na Rais Ruto.
“Rais Ruto anatujali ndio maana ameweka mikakati ya kumaliza usquota. Katika kipindi cha miaka mitatu pekee, serikali ya Rais Ruto imetumia zaidi ya Sh300 bilioni kutekeleza miradi mbalimbali ya maendeleo katika eneo la Pwani. Sasa tunahitaji nini zaidi?” alihoji.
Alisema kuchipuka kwa makundi haramu kama MRC ni kutokana na swala la uskwota.