NMG yazindua sera ya kuongoza matumizi ya AI katika uandishi wa habari
Kampuni ya habari ya Nation Media Group (NMG) imezindua sera maalum ya matumizi ya Akili Unde (AI) ili kuongoza matumizi ya teknolojia hiyo katika uandishi wa habari, ikiwa ya kwanza kufanya hivyo katika eneo hili.
Akili Unde (AI) ni mifumo ya kompyuta iliyobuniwa kufanya kazi ambazo kwa kawaida huhitaji akili ya binadamu. Kwa upande mwingine, AI ya kuzalisha maudhui ni teknolojia inayowezesha mashine kutengeneza maudhui mapya kulingana na data iliyotumika kuifundisha.
Tangu kuzinduliwa kwa apu ya ChatGPT na kampuni ya OpenAI mwaka 2022, zana za AI zimeenea kwa kasi katika utayarishaji wa maudhui na kuwa sehemu muhimu ya ubunifu wa kisasa.
Katika utangulizi wa mwongozo unaoitwa Mfumo Kazi wa Matumizi ya Akili Unde, Mhariri Mkuu wa NMG, Dkt Joe Ageyo anasema sekta ya uandishi wa habari haiwezi tena kupuuza teknolojia hiyo mpya.
“Kwa mashirika ya habari, swali si tena kama tutatumia AI, bali ni jinsi ya kuitumia kwa uwajibikaji, kimkakati na kwa njia itakayoongeza imani ya umma,” anasema.
Dkt Ageyo anasisitiza kuwa AI ni nyenzo ambayo wafanyakazi wa NMG wanaweza kutumia kuimarisha ubora wa habari katika majukwaa ya uchapishaji, kidijitali na matangazo.
“Kwa kuepusha shaka, tunatumia AI kuongeza kina, upeo na athari ya uandishi wetu wa habari, wala si kuchukua nafasi ya maamuzi ya kibinadamu, ubunifu na uwajibikaji uliotambulisha uandishi wa habari wa NMG kwa zaidi ya miongo sita,” anaeleza.
Mwongozo huu mpya unatarajiwa kufanya kazi sambamba na sera ya uhariri ya NMG ambayo tayari inasimamia kazi zote za uandishi wa habari katika shirika hilo.
“Mwongozo huu unaelekeza tu namna ya kutumia AI na hauchukui nafasi ya sera ya uhariri ya NMG, ambayo ndiyo mamlaka kuu ya uandishi wa habari ndani ya kampuni,” anaongeza.
Aidha, anasema mwongozo huo umeundwa kwa namna inayoweza kubadilika na utarekebishwa mara kwa mara kadri teknolojia ya AI inavyoendelea kukua.
Kutolewa kwa sera hiyo kunaashiria azma ya kampuni hiyo kuendana na mabadiliko ya kiteknolojia huku ikiendelea kudumisha imani ya hadhira kupitia matumizi ya AI kwa njia ya uwajibikaji na maadili.
Sera hiyo mpya pia inasisitiza ushiriki wa binadamu katika kazi zote za kampuni. Hii ina maana kuwa wahariri na wanahabari wataendelea kuwa na udhibiti wa mwisho katika upangaji, utayarishaji na uchapishaji wa maudhui, huku zana za AI zikitumika kuwasaidia.
Chini ya mfumo huo, wasomaji na watazamaji watajulishwa kila mara AI itakapotumika kuandaa maudhui, kukusanya data zao au kubinafsisha uzoefu wao wanapotumia bidhaa za NMG.
Sera hiyo pia inaweka masharti madhubuti ya kulinda data na faragha ya hadhira kwa kufuata kanuni za ndani za kampuni, sheria za Kenya, maadili ya vyombo vya habari na viwango vya kimataifa.
Vilevile, mfumo huo unaelekeza wanahabari maeneo ambayo AI inaweza kutumika, ikiwemo kutafsiri maudhui, kupanga habari, kuchambua hadhira, kuimarisha ushiriki wa wasomaji, kurahisisha baadhi ya kazi za kawaida na kusaidia matangazo lengwa.
Hizi ni baadhi ya shughuli za kawaida katika vyombo vya habari ambazo zinaweza kufanywa kwa ufanisi zaidi kupitia teknolojia.
Kuhusu uwezo wa wafanyakazi kutumia AI, mfumo huo pia unaeleza maeneo muhimu ya mafunzo kwa wafanyakazi, yakiwemo uelewa wa AI na data, kufikiri kwa kina, uhakiki wa ukweli, maadili ya matumizi ya teknolojia na kuelewa mahitaji ya hadhira.
Sera hiyo inaweka misingi 10 muhimu ya matumizi ya AI katika uandishi wa habari wa NMG, ikijumuisha uwajibikaji, usawa, ulinzi wa data, usalama wa mifumo ya AI, uwazi na uwezo wa kueleza namna teknolojia hiyo inavyotumika.
Mwongozo huu unaweka NMG miongoni mwa mashirika ya habari yanayoongoza katika matumizi ya AI kwa uwazi na uwajibikaji.
Kwa kufanya hivyo, kampuni hiyo yenye makao yake Nairobi sasa imejiunga na mashirika makubwa ya habari duniani yaliyoanzisha sera za matumizi ya AI, yakiwemo CNN, The New York Times, BBC, The Guardian, Financial Times na Sky News.
Hatua hii pia inajiri wakati ambapo Kenya inaendelea kuunda sera ya kitaifa ya AI kupitia mkakati wa Kitaifa wa AI 2025–2030, unaolenga kuongoza matumizi ya teknolojia hiyo nchini.