Habari

Mwanafunzi afariki, 10 wajeruhiwa tanki lilipoporomoka wakitazama msafara wa Ruto

Na BARNABAS BII March 12th, 2026 Kusoma ni dakika: 1

MWANAFUNZI mmoja alifariki dunia na wengine 10 wanaendelea kutibiwa hospitalini baada ya tanki la majitaka kuporomoka katika shule ya watoto wenye matatizo ya kusikia ya Kapsabet Alhamisi asubuhi.

Tukio hilo lilitokea wakati wanafunzi walikusanyika kuangalia gari la Rais William Ruto likielekea shule jirani ya upili ya wasichana ya Kapsabet.

Kamanda wa Polisi wa Nandi Central Maurice Okul, alithibitisha kuwa mwanafunzi aliyejeruhiwa vibaya alifariki akiwa hospitalini.

“Mwanafunzi aliyejeruhiwa alikufa katika hospitali ya Rufaa ya Kapsabet, huku wengine wakiendelea kupokea matibabu,” alisema.

Tukio hilo lilitokea wanafunzi waliposimama juu ya tanki la majitaka ndani ya shule huku wakisubiri kuona Rais. Shule hizo mbili zinagawanywa na barabara yenye upana wa chini ya mita tano.

Wafanyakazi wa dharura, walimu, polisi, na wakazi walijitokeza mara moja kuokoa wanafunzi waliofunikwa na mabaki ya tanki lililoporomoka.

Rais Ruto alifanya ziara ya ghafla katika shule hiyo na kutoa Sh5 milioni kusaidia kuboresha miundombinu ya shule.

“Tumehuzunishwa na tukio hili. Ni ahadi yetu kwamba tutasaidia wale walioumia,” alisema Rais.

Alielekeza serikali ya kaunti kuhakikisha miundombinu ya shule inaboreshwa, kwani wakazi wanasema haijakarabatiwa kwa muda mrefu.

Daktari Mkuu wa hospitali ya rufaa ya Kapsabet Richard Chepkwony, alisema wanafunzi 10 na waokoaji 5 waliopata majeraha wako katika hali nzuri.

Wanafunzi wawili walivunjika mifupa, huku wengine wakipata majeraha madogo. Waokoaji walijeruhiwa pia wakijaribu kuokoa watoto, lakini wote wako katika hali thabiti.