Huzuni mama akirejea kutoka kazini na kupata bintiye ameuawa
KILICHOTARAJIWA kuwa wikendi ya kawaida kwa Glorious Kaiza mwenye umri wa miaka 11 kiligeuka kuwa janga baada ya mtoto huyo kutoweka Jumamosi, na baadaye mwili wake kupatikana mapema Jumapili asubuhi ukiwa umefungwa ndani ya mfuko katika eneo la Mjambere, Kaunti Ndogo ya Kisauni, Mombasa.
Familia yake na majirani, ambao bado wameshtushwa na mkasa huo, walisema kuwa msichana huyo alipotea katika mazingira yasiyoeleweka.
Alikuwa nje akicheza na marafiki zake na ghafla akatoweka.
Wakati huo mama yake, Bi Elizabeth Barnabas, alikuwa ameenda katika shughuli zake za kawaida za kuuza uji ili kujipatia riziki.
Aliporudi nyumbani jioni aligundua kuwa binti yake hakuwepo.
Hali hiyo iliwafanya majirani kuanzisha msako uliodumu hadi usiku wa manane, walipoamua kutoa taarifa ya kupotea kwa mtoto katika Kituo cha Polisi cha Junda.
Kulingana na majirani, polisi waliwaomba warejee alfajiri.
Hata hivyo, jinamizi baya zaidi la Bi Barnabas lilitimia mapema Jumapili asubuhi pale mhudumu wa bodaboda alipomjulisha kuwa mwili wa mtoto ulikuwa umepatikana na polisi katika uwanja ulioko karibu kilomita mbili kutoka nyumbani kwake.
Alikimbilia eneo hilo na kuwakuta maafisa wa polisi wakichunguza eneo la tukio kabla ya kuthibitisha kuwa mwili huo ulikuwa wa binti yake aliyekuwa ametoweka.
“Aliyemuua binti yangu, kwa nini ulifanya hivyo? Nimekufanyia nini kibaya? Hili ni tukio la kutisha ambalo litaendelea kuniumiza milele,” alisema.
Jirani yake, Bi Habiba, ambaye pia alikuwepo wakati mwili ulipokuwa ukitolewa, alisema walimtafuta msichana huyo hadi saa sita za usiku kabla ya kuamua kuenda katika Kituo cha Polisi cha Junda kutoa taarifa ya tukio hilo.
Hata hivyo, waliambiwa na maafisa waliokuwa wakihudumu katika kituo hicho warudi nyumbani na kurejea alfajiri ili kurekodi taarifa rasmi.
“Nilipoamka Jumapili asubuhi, nilipokea simu kutoka kwa mtu aliyekuwa akielekea kanisani akiniambia kuwa mwili wa Gloria ulikuwa umepatikana. Niliogopa kumwambia mama yake kwa sababu wakati huo bado alikuwa analia bila kukoma na alikuwa ameathiriwa sana kwa kumpoteza mtoto wake,” alisema Bi Habiba.
Kamanda wa Polisi wa Kaunti Ndogo ya Kisauni Francis Muriithi, alipothibitisha tukio hilo, alisema mwili wa mwanafunzi huyo wa Gredi ya Tano katika Shule ya Msingi ya Buriani ulipatikana katika eneo la Manyani ukiwa umefungwa kwa blanketi na kuwekwa ndani ya mfuko wa kubebea bidhaa.
Maafisa wa upelelezi, wakishirikiana na vyombo vingine vya usalama, waligundua kuwa mwili huo ulikuwa umefungwa kitambaa machoni, huku mikono na miguu ikiwa imefungwa kwa kamba na kipande cha kitambaa kikiwa kimefungwa shingoni.
Pia walibaini kuwa vipande vya vitambaa vilikuwa vimejazwa mdomoni, vinavyoaminika kutumika kumziba mdomo mwathiriwa ili asipige kelele au kupiga mayowe.
Eneo la tukio lilirekodiwa na ushahidi muhimu kupatikana, ikiwemo madoa ya damu, kwa ajili ya uchambuzi zaidi.
Ingawa polisi wanasema ni tukio lisilo kawaida katika eneo hilo na wameahidi kuwa haki itapatikana, wakazi wanataka hatua zichukuliwe kuboresha usalama ambao wanasema umezorota katika eneo hilo.
Mwili wa msichana huyo ulipelekwa katika chumba cha kuhifadhi maiti cha Hospitali ya Rufaa ya Coast General ukisubiri kufanyiwa uchunguzi.