Mzozo: Iran sasa yalenga kufunga Bahari ya Shamu
TEHRAN, Iran:
BAADA ya kuzima shughuli katika Mkondo wa Hormuz, Iran sasa inaashiria kuwa inaweza kutumia washirika wake, Wahouthi nchini Yemen kufunga Mkondo wa Bab el-Mandeb ambayo ni ya kuingia Bahari ya Shamu.
Ikifaulu, Iran itatatiza biashara ya kimataifa na kusababisha bei ya mafuta kupanda hata zaidi.
Wachanganuzi wanasema Iran inalenga kuongeza shinikizo kwa Amerika kwa kudhibiti Mashariki ya Kati na Bahari ya Shamu.
Mkondo wa Bab el-Mandeb unaunganisha Bahari ya Shamu na Ghuba ya Aden, na ni njia muhimu inayotumiwa na meli nyingi za biashara pamoja na usafirishaji wa mafuta kutoka Saudi Arabia kuenda masoko ya dunia.
Jumatatu, afisa mmoja wa ngazi ya juu wa Yemen alionya kuwa majeshi ya nchi hiyo yako tayari kufunga mkondo huo ikiwa Saudi Arabia itaendelea kushambulia Yemen.
Alisema hatua hiyo inaweza kusababisha bei ya mafuta duniani kupanda hadi Sh25, 870 kwa pipa.
Mohammed al-Farah, mwanachama wa afisi ya kisiasa ya kundi la Ansarullah, maarufu kama Wahouthi, alidai kuwa Amerika inaichochea Saudi Arabia kuendelea na mashambulizi dhidi ya Yemen.
Alionya kuwa iwapo hali itaendelea kuwa mbaya, Mkondo wa Hormuz na Bab el-Mandeb zote zitafungwa.
Wataalamu wa masuala ya uchumi Mashariki ya Kati wanasema hatua hiyo itaathiri vibaya usafirishaji wa mafuta na bidhaa duniani.
Profesa Fawaz Gerges alisema Iran imeonyesha kuwa inaweza kutishia njia zote mbili muhimu za usafirishaji wa mafuta, jambo ambalo litazidisha mzozo wa sasa na kutishia ulimwengu mzima.
Wahouthi hapo awali walionyesha uwezo wao wa kuvuruga biashara ya kimataifa.
Baada ya vita vya Gaza kuanza mnamo 2023, walishambulia meli katika Bahari ya Shamuwakidai walikuwa wakilenga meli zinazohusishwa na Israel.
Mashambulizi hayo yalilazimisha kampuni nyingi za usafirishaji kubadilisha njia na kuzunguka Kusini mwa Afrika, jambo lililoongeza gharama za usafiri.
Mtaalamu wa usalama, Andreas Krieg, alisema Iran inaweza kutumia Wahouthi kulemea Amerika iwapo itaendelea kushambuliwa.
Naye Abdulaziz Sager wa Kituo cha Utafiti cha Ghuba alisema Wahouthi wana uwezo wa kuvuruga usafiri katika Bab el-Mandeb, lakini huenda wasichukue hatua hiyo bila amri ya Iran.
Ingawa hivyo, alionya kuwa jaribio lolote la kufunga njia hiyo linaweza kusababisha Amerika na washirika wake kuanzisha operesheni kubwa ya kijeshi dhidi ya Wahouthi.
Vita vinavyoendelea kati ya Amerika-Israel na Iran tayari vimeenea katika sehemu mbalimbali za Mashariki ya Kati, huku maelfu ya watu wakipoteza maisha, wengi wao raia wa Iran na Lebanon.