Makala

Wakulima Rift Valley wang’oa mahindi, majanichai na kukimbilia avokado

Na VITALIS KIMUTAI March 17th, 2026 Kusoma ni dakika: 2

WAKULIMA wanaomiliki mashamba madogomadogo katika kaunti kadhaa za Bonde la Ufa, wamegeukia kilimo cha parachichi almaarufu kama “dhahabu ya kijani kibichi” eneo hilo, baadhi waking’oa mazao yao ya mahindi na majanichai.

Soko la parachichi aina ya Hass katika masoko ya kimataifa limesababisha upanuzi wa kilimo cha parachichi katika maeneo mengi ya Bonde la Ufa yenye mazingira muafaka kwa zao hilo.

Baadhi ya wakulima wameacha kilimo cha mahindi na kukumbatia parachichi wakisema zao hilo lina faida zaidi.

Katika kaunti ya Bomet, eneo linaloongoza kwa kilimo cha majanichai kwenye mashamba madogomadogo na viwanda vikubwa, baadhi ya wakulima wanapanda majanichai pamoja na parachichi, wengine wanang’oa au kupunguza ekari wanazopanda majanichai wakisaka mbinu bora za riziki.

Eneobunge la Bomet Mashariki kwa sasa linaongoza kwa kilimo cha parachichi Bonde la Ufa Kusini, lakini maeneobunge mengine kama vile Konoin na Bomet ya Kati yamefuata mkondo vilevile kuhusu kilimo cha parachichi.

Mabadiliko sawa na hayo yameripotiwa katika kaunti jirani ikiwemo Narok, ambapo wakulima katika maeneobunge ya Narok Magharibi na Narok Kusini wamegeukia kwa wingi kilimo cha zao hilo.

Katika Kaunti ya Kericho, mabadiliko hayo yameshuhudiwa katika maeneobunge kama vile Kipkelion Mashariki, Soin Sigowet, Belgut na Bureti.

Aidha, katika Kaunti ya Nakuru, mkondo ni huo huo katika maeneobunge ya Kuresoi Kusini, Kuresoi Kaskazini na Rongai.

Richard Maritim, mkazi wa kijiji cha Mugango, Bomet ya Kati alisema alinunua miche 200 ya parachichi kutoka shirika la Isenya Roses, Kaunti ya Kajiado na akapata majuzi Sh200,000 kutokana na kilimo cha matunda hayo kupitia chama cha ushirika.

“Nililipwa Sh200,000 kwa zao hilo na ninatarajia mapato zaidi msimu ujao wa kuvuna. Siwezi kupata kiasi hicho cha pesa kutoka kwa shamba langu la ekari moja kwa mwaka mmoja, jambo linalofafanua sababu ya kuhamia kilimo cha parachichi,” alisema mkulima huyo wa avokado.

Hata hivyo, naibu mwenyekiti wa Halmashauri ya Majanichai Nchini Mhandisi Mosonik Menjo aliwarai wakulima wasing’oe mimea ya majanichai akisema mageuzi yanaendelea kuangazia sekta hiyo inayokumbwa na misukosuko.