Jinsi hifadhi za kijamii zinavyoendeleza biashara licha ya kusitishwa kwa ufadhili wa USAID
HIFADHI nyingi za wanyamapori za kijamii Kenya zimekuwa zikitegemea kwa kiasi kikubwa ufadhili wa wahisani kutoka nje ya nchi kuendesha shughuli, na kufuatia kusitishwa kwa ufadhili kutoka Shirika la Maendeleo la Kimataifa la Amerika (USAID), sasa zinatafuta mbinu mbadala kuendelea kusalia kwenye biashara.
Kenya ina karibu hifadhi 230 zilizosajiliwa na zinazokalia hekta milioni 9.04 kufikia Julai 2024.
Kulingana na Chama cha Hifadhi za Wanyamapori Kenya (KWCA), kusitishwa kwa ufadhili wa USAID mapema 2025 kuliacha pengo la Dola milioni 30 kwa kipindi cha miaka mitano, sawa na Dola milioni 6 kila mwaka zinazohitajika kuendesha shughuli za kibiashara.
Kuziba pengo hilo, hifadhi hasa zilizo maeneo kame na nusu-kame (ASAL) zinatumia mbinu mbadala na bunifu kujipatia mapato.
Hifadhi hizi ni za kijamii, makundi na za kibinafsi, na zina mchango mkubwa katika kulinda wanyamapori na kuboresha maisha ya wananchi.
Kwa mfano, Hifadhi ya Kiborit iliyoko katika Kaunti ya Baringo inakadiria kupoteza takriban Sh5 milioni ilizotarajia kutoka kwa USAID kusaidia shughuli kama vile ufugaji wa nyuki.
“Wanachama wengi hutegemea uzalishaji wa asali kujiendeleza kimaisha,” anasema naibu mwenyekiti wa hifadhi hiyo, Francis Tallam.
Hifadhi hiyo yenye ukubwa wa ekari 250 inasaidia zaidi ya maboma 500 yanayotegemewa kwa njia ya moja kwa moja na watu 1,500, na wengine 5,000 wanaoitegemea kwa njia isiyo ya moja kwa moja.
“Tulikuwa tunapanga kuweka mizinga 100 ya nyuki pamoja na kuzamia uchakataji wa asali, lakini kufuatia kusitishwa kwa USAID malengo hayo yamesimama,” Tallam anadokeza.
Kujiendeleza kibiashara, afisa huyo anasema hifadhi sasa imeingilia ufugaji wa kobe—biashara yenye faida, na anayoamini italeta mabadiliko makubwa kwa jamii za Kaunti ya Baringo ambazo kwa muda mrefu zimekumbwa na visa vya wizi wa mifugo na mashambulizi ya majangili.
“Tulipoanza kufuga kobe, tulipata oda kutoka Japan. Tunachoshughulikia ni leseni na vibali kuuza nje ya nchi,” alisema kwenye mahojiano. China, pia, ni soko lingine kubwa la kobe.

Shulmai, hifadhi ya kijamii iliyoanzishwa miaka minne iliyopita katika Kaunti ya Laikipia, pia, ilikuwa ikitegemea ufadhili wa USAID.
Mbali na shughuli za ufugaji kupitia paddocking, inajihusisha na uhifadhi wa rasilimali asilia, wanyamapori na bioanuwai (biodiversity).
“Wanachama wetu, hasa wanawake na vijana, wanajihusisha na utengenezaji wa shanga na ufugaji nyuki kujiendeleza kimaisha,” anasema meneja wa hifadhi hiyo, Johnson Saidimu.
Agosti 13 na 14, 2025 Chama cha Hifadhi za Wanyamapori Kenya (KWCA) kiliandaa Kongamano la Hifadhi za Kenya jijini Nairobi, jukwaa ambalo Shulmai ililitumia kuwasilisha wazo la ufadhili wa kujenga eneo la watu kujituliza na kujienjoi, maarufu kama eco-lodge.
“Eco-lodge ni mojawapo ya miradi ya kibiashara kuvutia watalii,” Saidimu aliambia Taifa Dijitali kwenye mahojiano ya kipekee, akieleza kuwa kuanzishwa kwa eco-lodge kutaongeza vyanzo vya mapato, huku hifadhi hiyo ikithamini wanyamapori wanaovutia watalii wa ndani kwa ndani na wa kimataifa.
Hifadhi hiyo imesitiriwa na shamba lenye ukubwa wa hekta 8,000 lililosajiliwa kama ardhi ya kijamii, ambapo baada ya majadiliano, jamii ilikubali kutenga hekta 6,000 kwa ajili ya hifadhi.
Hifadhi hiyo inanufaisha wanachama 1,211 kwa njia ya moja kwa moja na kwa njia isiyo ya moja kwa moja, huku baadhi ya wakazi wakijihusisha pia kwenye biashara ya uuzaji maji.
Kwenye Makala ya Pili ya Kongamano la Hifadhi za Kenya kaulimbiu yake ikiwa “Kufungua Uwekezaji kupitia Uhifadhi Endelevu”, Mkurugenzi Mkuu wa KWCA, Dickson Kaelo, alisema licha ya pengo la Dola milioni 30 lililosababishwa na kusitishwa ghafla kwa ufadhili wa USAID kwa kipindi cha miaka mitano, hifadhi nchini zinahitaji angalau Dola milioni 4 hadi 5 kila mwaka kwa muda wa miaka 10 hadi 15 ijayo ili kuendesha shughuli.
Kati ya zaidi ya hifadhi 230, Kaelo alisema karibu 39 sasa zimekumbatia mbinu mbadala kujipatia mapato ili kuendeleza shughuli zao na kupunguza utegemeaji wa wafadhili.
“Katika Kongamano la 2025, tulilenga kuangazia fursa za uwekezaji ambazo hifadhi zinapaswa kutathmini. Idadi kubwa iko kwenye utalii wa ikolojia, na tunahimiza wengine kufuata mkondo huo,” alisema, akizihimiza serikali za kitaifa na kaunti kuongeza ufadhili.
Hifadhi kama Mara, Amboseli, Ol Pejeta, Lewa, Loisaba na Borana—nyingi zikiwa karibu au ndani ya maeneo ya mijini na zenye wanyamapori, zinaendelea kusaka mbinu mbadala kujipa mapato.

Kwa mfano, Kituo cha Utafiti cha ILRI Kapiti na Hifadhi yake ya Wanyamapori, kinajihusisha na utafiti wa mifugo kwa kutumia ng’ombe, kondoo, mbuzi na ngamia.
“Lengo letu kuu sasa ni kufanya utafiti wa mifugo na kupatia jamii mifugo wanaostahimili mabadiliko ya tabianchi, afya bora ya wanyama, majaribio ya chanjo, utangamano kati ya mifugo na wanyamapori, ukuzaji nyasi na usimamizi bora wa malisho,” anasema Nehemiah Kimengich kutoka hifadhi hiyo ya Machakos.
Ingawa kituo hicho kinategemea ufadhili wa Taasisi ya Kimataifa ya Utafiti wa Mifugo (ILRI), Kimengich anakadiria kuwa karibu asilimia 10 ya ufadhili wao wa kimataifa uliathirika kutokana na kusitishwa kwa ufadhili wa USAID.
Ili kuziba pengo hilo, Kapiti sasa imezamia biashara ya utalii wa ikolojia na uzalishaji wa malisho ili kuboresha chakula cha mifugo.
Kwa kuwa jamii nyingi za wafugaji hutegemea hifadhi kulisha mifugo wao, hasa wakati wa kiangazi na ukame, baadhi ya hifadhi sasa zinaanza kunufaika na mikopo ya kaboni, kulingana na Vishal Shah, Mkurugenzi Mkuu wa Northern Rangelands Trust.
“Hifadhi nyingi hutegemea sana ufadhili kutoka nje, na kufuatia kujiondoa kwa wafadhili wakuu kama USAID, zinapaswa kuwa bunifu. Mbali na kujenga eco-lodge, tumeona baadhi zikijipatia mapato kupitia miradi ya kuhifadhi kaboni ardhini—kwa kuuza mikopo ya kaboni inayotokana na usimamizi bora wa nyasi,” anaeleza Shah.
Anafichua kuwa shirika lake lina wanachama 22 wa hifadhi wanaopata mapato kupitia uuzaji wa mikopo ya kaboni, sekta mpya inayolenga kusaidia jamii kukabiliana na athari za mabadiliko ya tabianchi.