Maoni

Mayatima wa Raila sasa ni mateka wa kisiasa wa Ruto: Wanamtegemea kusalia kazini

Na DOUGLAS MUTUA May 25th, 2026 Kusoma ni dakika: 2

AJABU iliyoje kwamba, mayatima wa kisiasa wa marehemu Raila Odinga sasa wamekuwa mateka wa kisiasa wa Rais William Ruto!

Baadhi yao wanamtegemea Dkt Ruto ili kusalia kazini; baadhi yao wanapumua pumzi za mwisho kisiasa.

Ikiwa Dkt Ruto alicheza kamari ya kisiasa na kuhakikisha mambo yako jinsi yalivyo, yaani yeye ndiye wa kutegemewa na mayatima hao, basi inabidi tumvulie kofia.

Kila Mkenya sasa amejua kuwa wale walioitwa wataalamu, ambao Dkt Ruto aliteua mawaziri kutoka kilichokuwa chama cha Bw Odinga, Orange Democratic Movement (ODM) si wataalamu wa chochote!

Utaalamu wa Waziri wa Kawi, Bw Opiyo Wandayi, na mwenzake wa Fedha, Bw John Mbadi, umefichuliwa kuwa butu na bandia na matukio ya hivi majuzi kama vile misukosuko ya bei za mafuta na mgomo wa magari ya usafiri wa umma.

Ni wazi kwamba, wawili hao wanamtegemea Dkt Ruto ili kutekeleza majukumu yao.

Ama ulielewaje waliposhindwa kudhibiti hali wakati wa misukosuko hiyo? Ilibidi Rais Ruto atafute suluhisho akiwa ugenini ndio bei za mafuta zipunguzwe na mgomo uishe.

Kila wakati mkubwa wako anafanya kazi ambayo amekuajiria, basi jua ama uko karibu kufutwa kwa kuwa huduma zako hazihitajiki, au mkubwa wako anafurahia udhaifu wako kwa kuwa unamtegemea sana, hivyo huna uhuru wa kumkosoa wala kushupaa shingo.

Kumbuka mawaziri hao walikuwa wabunge kabla ya kupewa kazi zao za sasa na Dkt Ruto.

Kutokana na udhaifu walioonyesha, nina hakika hata Dkt Ruto akiwafuta kazi leo, kisha waamue kurejea katika siasa, hawatafaulu.

Watakumbushwa kuwa wameshindwa na kazi.

Kumbuka tayari Bw Mbadi ameanzisha vita vya maneno na familia ya Bw Odinga, ambayo hudhibiti siasa za eneo la Nyanza, hivyo hata jaribio la kupewa tiketi ya chama cha ODM ili awanie cheo chochote ni ndoto.

Bw Mbadi alitamka maneno yaliyoonekana kutomheshimu marehemu Raila, jambo ambalo lilikasirisha familia hiyo.

Alianzisha vita vya maneno na dadake Raila, Bi Ruth Odinga, na pia akamkosea heshima binti ya mwendazake huyo, Bi Winnie Odinga.

Ni sahihi na salama kusema Bw Mbadi anaweza kuzika katika kaburi la sahau ndoto yake ya kurejea kwenye siasa.

Kuna makosa ambayo huwezi kusamehewa na familia ya marehemu Raila na wafuasi wao.

Bw Wandayi naye, japo ni jamaa ya Raila, hawezi kusimama mbele ya watu akaringia utaalamu wake! Usishtuke ukiwaona wakinyenyekea na kumsujudia Rais kwa jinsi ya kutia aibu.

Hivyo ndivyo teuzi za kisiasa zilivyo. Ukiweza, ziambae kama ukoma.