Afya na Jamii

Kushiriki mapenzi mara kwa mara huimarisha ubora wa mbegu za kiume – Utafiti

Na CECIL ODONGO March 27th, 2026 Kusoma ni dakika: 1

KUSHIRIKI tendo la ndoa mara kwa mara husaidia kuimarisha ubora wa mbegu za kiume, Utafiti mpya umebaini.

Utafiti huo umezima kabisa dhana kuwa kukaa kwa muda mrefu bila kushiriki mapenzi na kuwa na mbegu kadhaa za kiume, husababisha mbegu hizo kuwa bora na imara zaidi.

Jarida la The Conversation lililochapisha utafiti huo, ambao sasa unawashauri wanaosaka watoto kuhusu ubora wa mbegu za kiume na wakati bora zaidi wa kujaamiana.

“Kwenye uchunguzi wetu, tulikusanya data ya shahawa kutoka kwa machapisho ya tafiti 115 za awali ambapo wanaume 55,000 walihusika. Tulibaini kuwa wanaume wasiposhiriki ngono, afya ya mbegu zao za kiume hudorora na uwezo wa mbegu hizo kutoka sehemu moja hadi nyingine hupungua. Chembechembe za DNA kwenye mbegu za kiume pia huharibiwa,” unaeleza utafiti huo.

Hata hivyo, utafiti huo ulibaini kuwa kukosa kushiriki mapenzi huongeza idadi ya mbegu za kiume ila wingi pekee si kigezo tosha cha ubora wa mbegu za kiume.

Kwa hivyo, mbegu za kiume ambazo zimehifadhiwa kwa miaka kadhaa kutokana na mwanaume kutoshiriki ngono hupungua ubora na makali ya kutungisha mimba.

Utafiti huu umetolewa wakati ambapo vijana wengi hawaonekani kushughulishwa na ndoa au mahusiano ya kimapenzi.