Hali zinazochangia ujauzito kuharibika
ALIPOPATA ujauzito wake wa kwanza, Phidilia Kibirisho Mwendwa na mumewe walikuwa na furaha tele.
Walifanya maandalizi yote ya kumpokea kifungua mimba.
Walimnunulia malaika huyu nguo, wakapanga tarehe ambayo angebatizwa kanisani na hata kutangaza taarifa kuwa walikuwa wanamtarajia mwanao kwa marafiki na jamaa waliokuwa mbali nao.
Hata hivyo, furaha hiyo iligeuka kuwa huzuni mwingi baada ya kuupoteza ujauzito wake katika wiki ya 29.
“Nilianza kuhisi maumivu makali sana kisha mume wangu akanipeleka hospitalini lakini kwa bahati mbaya, mtoto wangu alipatikana akiwa ameshaaga tumboni na hivyo madaktari walimtoa akiwa maiti,” Phidiliah anasimulia kwa huzuni.
Miezi iliyofuata, Phidilia na mumewe walimuomboleza mwanao. Ilikuwa vigumu pia kwao kuyajibu maswali ya marafiki na jamaa waliokuwa wakiwauliza jinsi mtoto alivyokuwa akiendelea bila kujua alikuwa ameaga.
“Mume wangu alikuwa akinifariji mara nyingi sana. Wakati mwingine angenipata nikiwa chumbani nimeshikilia zile nguo tulizokuwa tumemnunulia mtoto wetu kabla ya kuzaliwa lakini angenielewa. Majonzi ya kumpoteza mtoto wetu yaliponizidi, nilimuomba tuhamie nyumba nyingine ya kukodisha na kugawa zile nguo tulikuwa tumemnunulia mtoto wetu aliyeaga dunia na aliniunga mkono.”
Miezi iliyofuata, walibahatika tena kupata ujauzito mwingine, lakini kwa bahati mbaya tena walimpototeza alipofikisha wiki ya nane ya ujauzito.
“Damu ilianza kutoka kwa uchungu sana na tulipofika hospitalini, daktari aliniambia kuwa nilikuwa nampoteza mtoto wangu na hakuna kitu hospitali ingefanya kumuokoa. Nilijiuliza maswali mengi sana, lakini sikupata majibu.”
Phidilia anasema kuwa safari yake ya kuitwa mama ilizidi kuchelewa kwani kadri alivyopata ujauzito, ndivyo alivyozidi kupoteza wanawe.
Baada ya kuupoteza ujauzito wa wiki 30, anasema kuwa alimuuliza daktari wake kwa sauti ya unyonge ikiwa kuna siku ataitwa mama.
“Niligundua kuwa nilikuwa na ujauzito wangu wa nane katika wiki ya sita. Baada ya kupigwa picha, daktari wangu aliniambia kuwa huo ujauzito haukuwa salama kwani ulikuwa unatingika. Niliwekwa kwenye matibabu na kuruhusiwa kurudi nyumbani lakini siku mbili baadaye, nilikuwa navuja damu. Mume wangu alinirudisha hospitalini na kwa bahati mbaya, niliupoteza ujauzito huo tena,” anasema Phidilia.
Siku moja rafiki wake alimshauri kubadilisha daktari wa uzazi wa kina mama. Ushauri ambao aliuzingatia. Siku zilizofuata, alihusishwa kwenye ushauri na mmoja wa madaktari hao.
Miongoni mwa mawaidha aliyopewa yalikuwa ni mumewe kumpeleka kwenye likizo sehemu anakopenda ili apumzike, mbali na mazingira ambayo alikuwa ameyazoea.
Pia aliambiwa kuwa atoe kwenye fikra wazo la kutaka kumpata mtoto.
“Ama kweli ushauri huo ulizaa matunda kwani niligundua nilikuwa mjamzito mara ya tisa. Lakini badala ya kuwa na furaha, nilihofia kuwa nitaupoteza tena ujauzito ule. Siku hiyo daktari wangu aliniambia kuwa nitambeba mwanangu mkononi na kumnyonyesha.”
Ujumbe huo ulimpa matumaini pamoja na mumewe japo wanasema kuwa safari ya ujauzito huo ilikuwa ghali mno.
“Niliwekwa kwenye muda wa mapumziko na matibabu naye daktari wangu wa uzazi alikuwa akiniangalia kila Jumamosi. Wakati wa usafiri, mume wangu pekee yake ndiye alikuwa dereva ilikuhakikisha kuwa sitingiki kwenye barabara,” anaeleza.
Uangalifu huo wa hali hiyo ya juu na madaktari wawili wa uzazi walioshauriana jinsi ya kuhakikisha kuwa Phidilliah hapotezi tena ujauzito huo ulizaa matunda.
“Nilipofika wiki ya 29 na siku 3 ya ujauzito, nilijifungua mtoto wangu wa kwanza. Alikuwa na kilo 2.7 na kuwekwa kwenye mashini ya watoto ambao wamezaliwa kabla ya siku zao kutimia. Siku 14 baadaye, nilipopewa mtoto wangu mkononi ndipo niliamini kuwa nimekuwa mama mzazi,” anaeleza kwa tabasamu.
Ujio wa malaika huyo ulirahisisha ujio wa watoto wengine wawili miaka iliyofuata na sasa, Phidilia ni mama wa watoto watatu walio na umri wa miaka 12, 8 na 3.
“Jambo la kufurahisha ni kuwa ujauzito wangu wa mtoto wangu wa pili ambaye ni wa kiume haukuwa na changamoto yoyote. Alizaliwa akiwa na kilo 3.8 bila upasuaji na sasa ni mtoto ambaye ni mchangamfu,” anasimulia.
Hali sawia ilimpata Mactilda Makana. Alipoingia kwenye ndoa mwaka wa 2008. Anasema kuwa alijua kuwa kuitwa mama si jambo la kusubiria.
Hata hivyo, hali ilibadilika baada ya kupoteza ujauzito mara tano zilizofuatana.
“Mimba ya nne nilibeba hadi miezi saba kisha nikampoteza mtoto huyo. Kisha ya tano nilibeba ujauzito hadi siku ya kujifungua lakini nilimpoteza muda mfupi baadaye,” anasimulia kwa uchungu.
Mactilda anasema kuwa baada ya visa hivyo vilivyofuatana vya kuwapoteza watoto vilichangia ndoa yake kuvunjika.
“Mume wangu na wazazi wake waliniambia kuwa hawangeendelea kuishi na mwanamke ambaye hawezi kubeba ujauzito na kuzaa watoto walio hai. Nilitoka kwenye ndoa hiyo ya miaka minne nikiwa na msongo mwingi sana wa mawazo,” anakumbuka Mactilda.
Anasema kuwa alitumia muda huo mgumu kuomba Mungu kila mara. Kwa wakati mmoja, aliandika barua akiomba dua ya kuitwa mama na kuipeleka kanisani ili aombewe. Na ombi hilo lilijibiwa kwanza alipofunga ndoa tena na kisha kupata ujauzito.
“Katika mimba za awali sikuwa napata ushauri wa daktari wa uzazi. Lakini wakati tu niliingia kwenye ndoa ya pili, nilipata ushauri wa daktari wa uzazi hata kabla ya kupata ujauzito. Hatua hiyo ilinisaidia hadi wakati ambapo nilijifungua pacha wangu ambao kwa sasa wana miaka sita,” anaeleza kwa tabasamu.
Kulingana na mkuu wa huduma za matibabu spesheli ya uzazi, Dkt Ong’ech Odero, kuna visa vingi nchini vya wanawake kupoteza ujauzito.
Anasema kuwa changamoto za kiafya kama vile ugonjwa wa kisukari, shinikizo la damu, changamoto na sehemu ya uzazi wa mama au hata baadhi ya virusi na bakteria zinazosababishwa kingono vinaweka mwanamke mjamzito katika hatari ya kumpoteza mwanawe kabla ya kujifungua.
“Visa vya wanawake kupoteza ujauzito pia viko juu miongoni mwa wanawake ambao wametimu umri wa miaka 35 na zaidi. Pia hali ya maisha na mazingira kama vile uvutaji sigara, baadhi ya kemikali hatari na utapia mlo pia zinachangia hatari ya mwanamke kuupoteza ujauzito,” anasema Dkt Odero.
Dkt Odero pia anaeleza kuwa shughuli za kawaida kama mazoezi, tendo la ndoa, uchovu wa akili unaotokana na kazi za kila siku na visa vidogo vya kuanguka havimweki mjamzito katika hatari za kumpoteza mtoto.
“Tafuta ushauri wa kiafya kwa muuguzi endapo unatoa damu, ukiwa na maumivu makali chini ya tumbo, au unapozimia wakati ukiwa mjamzito,” akaongeza Dkt Odero.
Naye mwanasaikolojia, Ann Arithi Munyao, anasema kuwa kupoteza ujauzito huwa jambo zito na huathiri mwanamke anayeomboleza.
“Huu huwa wakati mgumu sana na mara nyingi unapata wanawake wanajilaumu kuwa wangefanya mambo tofauti huenda halingetendeka. Kuzungumzia ujauzito uliopotea ni ngumu sana kwa sababu si jambo ambalo linazungumziwa hadharani na wakati mwingine jamii huhukumu wanawake waliopoteza ujauzito,” anaongeza Ann.