Dimba

Jinsi Senegal imepanga kupigana kuhifadhi AFCON waliyoambiwa waipe Morocco

March 27th, 2026 Kusoma ni dakika: 1

Shirikisho la Soka la Senegal Jumatano jioni liliwasilisha rasmi rufaa yake kwa Mahakama ya Kutatua Mizozo ya Michezo (CAS) kuhusu aumuzi wa CAF wa kuwapokonya Kombe la Afrika (AFCON 2025)

Rufaa hiyo itasikizwa na CAS ambayo ina makao yake Uswizi. Matokeo ya fainali hiyo yalibadilishwa kwa njia tata na kusababisha Senegal wakate rufaa kupinga uamuzi huo.

CAF ilitoa uamuzi kuwa Senegal ilipoteza mechi hiyo ya fainali mnamo Januari 18 baada ya kuondoka uwanjani kabla ya mchezo kukamilika. The Lions of Teranga waliondoka uwanjani baada ya Morocco ambao ndio walikuwa wenyeji kupewa penalti mechi ikielekea kukamilika.

Waliondoka uwanjani kwa dakika 14 kabla kurejea na kuendelea na mechi ambapo waliwahi ushindi wa 1-0.

Bodi ya kutatua mizozo kwenye CAF wiki jana ilibadilisha matokeo kwa kuwapa Morocco ushindi wa 3-0

“Shirikisho la Soka Senegal limekata rufaa kuhusu uamuzi huo ikisisitiza kuwa ubingwa huo ni wao na hauendi popote. Tunahitaji mahakama iweke kando uamuzi wa CAF na watangazwe mabingwa,”

“Pia inaomba kuondolewa kwa makataa ya muda wa kuwasilisha rufaa hadi uamuzi wa CAF na hoja zilizoibuliwa ziangaziwe,” ikasema taarifa ya CAS.

Kamati ya kusikiza rufaa ya Senegal kwenye CAS itateuliwa na kutakuwa na mwongozo wa kina kuhusu kusikizwa kwa kesi yote.

Serikali ya Senegal awali ilikuwa imetoa wito uchunguzi ufanywe kuhusu kupokonywa kwao taji.

Mawakili wa Shirikisho la Soka Senegal walitarajiwa kutoa taarifa kuhusu suala hilo baadaye jana.

Baada ya Senegal kupokonywa ubingwa huo kulikuwa na malalamishi kotekote kuhusu kupuuzwa kwa ripoti ya refa ambaye aliamua mchezo uendelee hada baada ya Senegal kuondoka uwanjani.

Wadadisi wa masuala ya soka walihoji kwamba Senegal hawakustahili kuadhibiwa kwa kupokonywa taji kwa sababu ni refa aliyewaruhusu warejee uwanjani na kuendelea na mchezo.