Dimba

Misri wafokea Fifa kwa ‘ukora’ katika mechi dhidi yao na Argentina

Na MASHIRIKA July 8th, 2026 Kusoma ni dakika: 2

KOCHA wa Misri Hossam Hassan amesema hana nia ya kutazama mechi zilizosalia za Kombe la Dunia akisema refa alichangia timu hiyo kubanduliwa na Argentina mnamo Jumanne usiku.

Katika mechi nyingine, Uswizi walibandua Colombia 4-3 kupitia mikwaju ya penalti na kufuzu robo fainali.

Timu hizo zilikuwa zimeagana sare tasa muda wa kawaida na ule wa ziada kabla ya kuamuliwa na mikwaju ya penalti.

Sasa Argentina na Uswizi zitachuana katika robo fainali wikendi hii huku Misri na Colombia zikiaga kombe.

Misri walikuwa wakiongoza 2-0 zikiwa zimesalia dakika 11 mechi iishe katika raundi ya 16 dhidi ya Argentina.

Kwa masikitiko walifungwa mabao matatu na ikabidi waage mashindano hayo ya hadhi ya soka.

Mshambuliaji nyota wa Argentina Lionel Messi ashangilia kufunga bao la kusawazisha dhidi ya Misri katika mechi ya 16-bora uga wa Atlanta, jimbo la Georgia, Amerika, Julai 7, 2026. Argentina ilishinda mechi 3-2. Picha|Reuters

Mkongwe Lionel Messi aling’ara katika mechi hiyo na kutumia uweledi wake kuhakikisha Argentina inatinga robo fainali.

Hassan alilalamika kuwa walionewa na hana nia ya kutazama mechi zilizosalia za kombe la dunia.

“Naenda nyumbani na sitatazama mechi hizo kwa sababu kilichotutendekea si haki. Tulistahili kupewa penalti, bao letu lilikataliwa na sijui kwa nini lilikataliwa,” akasema akionekana mwenye hasira.

Egypt walifunga bao dakika ya 62 kupitia Mostafa Zico lakini VAR iliangalia na kutambua kuwa kulikuwa na mpira wa ikabu kwa Argentina kuelekea kufungwa kwa bao hilo.

Pia Misri walilia kwamba walistahili kupewa penalti baada ya Hamdy Fathy kuangushwa ndani ya kijisanduku.

Hasira yao ilipanda kwa kuwa baada ya tukio hilo kwa kuwa Argentina waliendelea kucheza na kufunga bao dakika ya 92 kupitia Messi.

“Mimi huwa sipendi kushindwa na kama kupoteza kwangu kumechangiwa na refa jinsi ilivyofanyika hivi leo, nawaambia tu mashabiki wetu wasikasirike. Tulicheza vizuri sana na kushindwa kwetu kumechangiwa na refa,” akaongeza.

Hassan alisema alifurahi kuwa wachezaji wake walifuata mwongozo wake mchezoni na waliwalemea Argentina.

Misri wamekuwa wakitumia mbinu ya kulinda ngome yao mchezoni lakini dhidi ya Argentina walikuwa wakivamia hasa kupitia mipira mirefu na pia pembeni.

Pia mnyakaji wao Mostafa Shoubir alionyesha uweledi wa juu baada ya kuokoa mikwaju hatari ya Argentina.

“Najivunia sana wachezaji wangu kwa sababu wengi wao wanacheza kwenye Ligi Kuu ya Misri nao wapinzani wetu walikuwa na wachezaji wanaoshiriki ligi za kifahari za Ulaya,” akaongeza.

Colombia nao watajilaumu wenyewe baada ya nyota wa Bayern Luis Diaz na wenzake kukosa nafasi kadhaa za kufunga na kumaliza mchezo mapema.

Kipa wa Uswizi Gregor Kobela aliokoa penalti ya Cucho Hernandez baada ya ile ya Davinso Sanchez kugonga mtambapanya kwa Columbia.

Manuel Akanji pia alikosa penalti kwa upande wa Uswisi.