Habari

Afueni baada serikali kusitisha mfumo wa ununuzi dijitali shuleni

Na MERCY SIMIYU March 28th, 2026 Kusoma ni dakika: 1

SHULE za umma zimepata afueni ya muda baada ya Wizara ya Fedha kuziruhusu kuendelea kununua bidhaa na huduma nje ya mfumo wa kielektroniki wa ununuzi wa serikali (e-GP), kufuatia kuchelewa kwa mafunzo kwa wakuu wa taasisi hizo.
Katika barua kutoka kwa Katibu wa Idara ya Uwekezaji wa Umma na Usimamizi wa Mali Cyrell Odede Wagunda, serikali ilikubali ombi la Katibu wa Elimu ya Msingi Julius Bitok la kutaka shule zipewe msamaha wa muda kabla ya kuhamia mfumo huo wa kidijitali.
Wakuu wa shule walipinga matumizi ya e-GP wakisema si rahisi kutekelezwa hasa katika maeneo ya mashambani ambako ununuzi hufanywa kutoka kwa jamii. Wazazi pia huchangia kwa kutoa bidhaa kama vyakula, kuni na hata kufanya kazi badala ya karo.
Wagunda alisema msamaha huo ni muhimu kwa kuwa shule hazijapewa mafunzo ya kutosha kutumia mfumo huo.
“Tumechunguza ombi la kuruhusu taasisi kununua nje ya mfumo wa e-GP. Kwa kuwa hatujaanzisha mafunzo, shule zinaweza kuendelea kununua nje ya mfumo huo hadi itakapotangazwa vinginevyo,” ilisema sehemu ya barua hiyo.
Profesa Bitok alikuwa ameomba mwongozo kuhusu iwapo shule zinaweza kuendelea kutumia njia za kawaida kwa muda. Nchini kuna zaidi ya shule za msingi 23,000 na sekondari 9,000 za umma.
Mfumo wa e-GP ulizinduliwa mwaka jana ukiwa jukwaa la mtandaoni la kurahisisha na kuongeza uwazi katika ununuzi wa umma. Unalenga kuboresha uwajibikaji na ufanisi katika hatua zote za manunuzi.
Hata hivyo, Wizara ilisisitiza kuwa licha ya msamaha huo, shule lazima zifuate kikamilifu Sheria ya Ununuzi wa Umma ya 2015.
Hatua hii inaangazia changamoto zinazoendelea katika kuhamia mifumo ya kidijitali kwenye sekta ya elimu, hasa kuhusu uwezo wa taasisi za masomo.
Mnamo 2024, serikali ililazimika kusitisha agizo la kulipa karo kupitia eCitizen baada ya kupingwa na wazazi na wasimamizi wa shule.