Dondoo

Lofa ashangaza kudai atafaulu kibiashara akiwa na babu yake ahera

Na KALUME KAZUNGU March 31st, 2026 Kusoma ni dakika: 1

SOSO-CHAMARI, Kilifi

LOFA mmoja mvutaji bangi mtaani hapa, alishtua wazazi wake alipoitisha kikao na kuwaaga akidai marehemu babu yake amemwalika.

Jombi anadai siku za hivi karibuni hajakuwa huru kwani kila anapolala humuona babu yake njozini akimwita wakashirikiane kibiashara.

Hivyo, lofa aliwaarifu babake na mamake kwamba wakati wake umefika.

Alisema raha anazoonyeshwa na babu yake njozini na anazofaa kwenda kukutana nazo hazina kifani.

Nduguye anayefahamu vyema tabia za kakake aliwaambia wazazi wake wampuuze.

“Msiyachukulie matamshi yake kwa uzito. Ni bangi tupu hiyo. Wachaneni na yeye. Msisononeke. Yuko kwa dunia yake huyo,” akaambia wazazi.