Maoni

MAONI: Kuhakiki sajili ya wapigakura kutaondoa ‘Tharaka-Nithi’ feki

Na CECIL ODONGO April 6th, 2026 Kusoma ni dakika: 2

JUHUDI ambazo Tume ya Uchaguzi (IEBC) inaendeleza kuhakikisha kuwa kila mpigakura amesajiliwa kupitia mfumo wa teknolojia wa biometriki zinastahili kuungwa mkono na wote badala ya kuingizwa siasa.

Tume hiyo kwa sasa inaendeleza usajili wa wapigakura kote nchini na mahamasisho yanaendelea kutoka kwa wadau mbalimbali kuhakikisha kuwa vijana wanajisajili.

Hata hivyo, tangazo la IEBC kuwa wapigakura waliojisajili kabla ya uchaguzi wa 2012 na maelezo yao hayakunakiliwa kupitia biometriki, limeibua tofauti kali kutoka kwa wanasiasa.

Mwanzo hata kabla ya kubishana, kila Mkenya anastahili kuthibitisha maelezo yake na IEBC ili afahamu iwapo atapiga kura au la.

Kupiga kelele mitandaoni na kuhusisha tangazo la IEBC na wizi wa kura hakutasaidia chochote kwa sababu bila utambuzi wa biometriki, hutaweza kupiga kura mwaka ujao.

Kwa hivyo, wanaopinga IEBC mitandaoni wapinge na wanaoiunga mkono wafanye hivyo lakini ulazima ni kujisajili kupiga kura au kuthibitisha unaruhusiwa kupiga kura.

Uongozi mbaya au nzuri huwekwa au kuondolewa madarakani kupitia kura. Kwa hivyo, vijana wa Gen-Z wajisajili ili wajiamulie mkondo wa taifa lao badala ya kuwategemea wanasiasa wakongwe.

Pili, sajili ya wapigakura lazima isafishwe kuhakikisha kuwa wale ambao wamejisajili ndio wanashiriki uchaguzi, na kura zinahesabiwa kwa haki.

Mbali na uchaguzi wa 2002, chaguzi nyingine ambazo zimeandaliwa tangu mwanzo wa mfumo wa vyama vingi, zimekuwa na maswali kuhusu uwazi wao.

Kumekuwa na maandamano, uharibifu wa mali na maafa kila baada ya uchaguzi huku walioshindwa wakilalamika kuwa kura zao zimeibwa.

Ni kupitia sajili ya wazi ya wapigakura ndiko kutamaliza ‘wafu’ kuondoka kaburini kisha kupiga kura kwa manufaa ya mwaniaji mmoja hata kama hana umaarufu wa maana.

Baadhi ya viongozi wa maeneo mengine nchini wamekuwa wakijishaua kuwa wanajivunia uungwaji mkono mwingi na jamii zao zina kura nyingi.

Msingi wa idadi ya juu au ndogo ya wapigakura upo kwenye takwimu ambazo mwishowe zitatolewa na IEBC na ndiyo itathibitisha kama kauli ya wanasiasa hawa ina mashiko yoyote.

Iwapo wamekuwa wakijivunia kura ya wafu, basi ole wao kwa kuwa sajili ya wapigakura inastahili kuwa na majina ya wale ambao wanaishi tu na kuzima ukora wa wizi wa kura.

Kile ambacho viongozi wanastahili kufanya iwapo wanataka kusalia uongozini na wale wanaotaka kuchukua serikali, ni kushiriki mahamasisho mengi ya kuwashaajisha wafuasi wao wajisajili na wathibitishe maelezo yao na IEBC.

Huu ndio wakati wa kupata idadi ya juu ya wapigakura kwa kuhakikisha wengi wanajisajili mno ili hatimaye wakupigie kura na uchaguliwe 2027.

Ukweli ni kuwa usajili wa wapigakura ni sehemu ya kupata ushindi wa mapema uchaguzini. Kibarua kinachofuata ni kuhakikisha kuwa waliojisajili wanajitokeza na kushiriki shughuli hiyo ya kikatiba.

Kwa vijana ambao wanasiasa wanalenga kura zao, huu ndio wakati wa kuhakikisha ‘wako kadi’ kama wanataka mabadiliko nchini.

Wafahamu kuwa siasa za maandamano hazichangii mabadiliko jinsi wanavyokusudia bali kuwaweka viongozi wachapakazi kwenye nafasi za uongozi ndiko kutawasaidia.

Siasa za Kenya zimeingizwa ukabila na vijana wasipochunga wanasiasa watateka nyara baadhi ya maazimio yao na kuyatumia kuendeleza maslahi yao ya kibinafsi.

Gumzo kwa sasa linastahili kuwa sote tunajisajili kupiga kura kwa kuwa hilo ndilo litadumisha uongozi wa sasa au kuuondoa badala ya siasa za chuki na kurushiana matusi mitandaoni.